Biteko azindua App mpya kuwajengea uwezo wahandisi 

September 25, 2025 1:17 pm · Kelvin Makwinya
Share
Tweet
Copy Link
  • ERB-Mhandisi App itawawezesha wahandisi na wadau kupata taarifa muhimu ikiwemo kuhakiki uhalali wa wahandisi wa miradi, kulipia ada, kupata taarifa za miradi, kuhakiki taarifa binafsi pamoja na kuripoti taarifa hatarishi.

Dar es Salaam. Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko, amezindua rasmi  programu tumishi (application) ya ERB-Mhandisi, mfumo mpya wa kidijitali utakaorahisisha huduma mbalimbali za kihandisi ikiwemo kupata taarifa za miradi.

Uzinduzi huo umefanyika leo Septemba 25, 2025 jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 22 wa Mwaka wa Wahandisi, ambapo Dk. Biteko alikuwa mgeni rasmi akimuwakilisha Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Kwa mujibu wa Dk Biteko, ERB-Mhandisi App itawawezesha wahandisi na wadau kupata taarifa muhimu ikiwemo kuhakiki uhalali wa wahandisi wa miradi, kulipia ada, kupata taarifa za miradi, kuhakiki taarifa binafsi pamoja na kuripoti taarifa hatarishi.

Katika mkutano huo, ambapo zaidi ya wahandisi 400 wameapishwa, Dk. Biteko amesisitiza umuhimu na mchango mkubwa wa taaluma ya uhandisi katika maendeleo ya Taifa.

Kwa mujibu wa Dk Biteko, ERB-Mhandisi App itawawezesha wahandisi na wadau kupata taarifa muhimu ikiwemo kuhakiki uhalali wa wahandisi wa miradi, kulipia ada, kupata taarifa za miradi, kuhakiki taarifa binafsi pamoja na kuripoti taarifa hatarishi. Picha | Zanzibar News.

“Kwa wastani, taaluma ya uhandisi huzalisha kati ya Dola saba hadi kumi za Marekani kwa kila dola moja inayowekezwa. Aidha, zaidi ya asilimia 70 ya ubunifu mpya na teknolojia duniani unahusishwa na uhandisi, ukiwa unagusa sekta za tehama, nishati, viwanda na akili mnemba,” amesema Dk. Biteko.

Pamoja na kuzindua ‘App’ hiyo, Dk. Biteko ameitaka Bodi ya Wahandisi nchini kuongeza juhudi katika kuwaendeleza wahandisi vijana ili kupanua wigo wa wataalamu watakaoweza kushindana ndani na nje ya mipaka ya Tanzania.

“Wako wahandisi vijana wadogo ambao kila wakijaribu kufurukuta waonekane kuna nguvu kubwa sana inayotumika kuwashusha na kuwadidimiza badala ya kuwaruhusu wachipuke” amesema Dk Biteko. 

Aidha, amehimiza kuanzishwa kwa mfumo wa kutambua na kutoa motisha kwa wahandisi wanaotekeleza miradi kwa ubora, hatua ambayo itachochea ushindani na kuongeza weledi katika sekta hiyo.

Akihitimisha hotuba yake, Dk. Biteko ameeleza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wahandisi katika nyanja zote kwa lengo la kuboresha mazingira ya kazi na kurahisisha utekelezaji wa majukumu yao.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...