Airtel Tanzania yajitanua hadi SADC kwa huduma za kifedha kwa njia ya simu
- Wateja wake sasa wataweza kutuma na kupokea fedha Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).
- Lengo ni kuongeza ujumuishaji wa kifedha na kukidhi mahitaji ya wateja wake.
Dar es Salaam. Huenda watumiaji wa mtandao wa Airtel Tanzania waliokuwa wakihofia kukosa huduma ya kutuma na kupokea pesa nje ya nchi wakaanza kutabasamu baada ya changamoto hiyo kuondolewa.
Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania imezindua kampeni mpya katika huduma zake za Airtel Money ya “Africa Bila Mipaka” inayowawezesha wateja wake kutuma na kupokea fedha katika nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC)
Nchi hizo za SADC ambazo mteja wa Airtel Money ataweza kutuma na kupokea fedha ni Malawi, Zambia, Zimbabwe, Madagascar, Botwana, Lesotho na Namibia.
Kwa uzinduzi huo, Airtel imekamilisha kutoa suluhu ya huduma za kifedha kwa njia ya simu wa nchi zote za Afrika.
Mkurugenzi wa Huduma za Airtel Money Tanzania Isack Nchuda amesema mtandao huo wakati wote umekuwa ukitoa huduma bunifu zinazogusa maisha ya kila siku ya Watanzania.
“Huduma hii tunayozindua leo (Novemba 23, 2022) inawaunganisha wateja wetu wanaotumia simu kufanya miamala duniani na kuwezesha kufanikisha ndoto zao,” amesema Nchuda.
Aitel Money yazindua kampeni ya Afrika bila mipaka, kampeni inayowawezesha wateja wake kutuma na kupokea pesa kwenye nchi zilizo kusini mwa jangwa la Sahara kupitia akaunti zao za Airtel Money.#AfrikaBilaMipaka
pic.twitter.com/AZiDDnOPnl— Airtel Tanzania (@airtel_tanzania) November 23, 2022
Kwa mujibu kampuni hiyo ya mawasiliano, huduma hiyo salama na ya uhakika itapanua upatikanaji wa huduma za kupokea na kutuma pesa kwa njia ya simu mjini na vijijini.
“Tunaendelea kurahisisha kutuma pesa moja kwa moja kwenye akaunti za Airtel Money hapa nchini Tanzania kutoka nchi za SADC. Wateja wanaweza kupakua applikesheni au kutengeneza akaunti ili kuanza kutumia huduma hii na kuanza kutuma au kupokea fedha kwa familia na marafiki,” amesema Nchuda.
Soma zaidi:
-
Thamani miamala ya kifedha kwa njia ya simu yapungua, watumiaji wakiongezeka
Licha ya Serikali kuweka tozo katika miamala ya kifedha kwa njia ya simu, huduma hizo zimesaidia kuongeza ujumuishaji wa kifedha kwa wananchi, kupunguza muda wanaotumia kwenda benki na kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi.
Airtel Money Tanzania kwa sasa imeunganishwa na kampuni zaidi ya 1000 na taasisi zaidi ya 40 za kifedha.
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), hadi kufikia Septemba mwaka huu, Airtel Money ilikuwa na watumiaji milioni 8.9 sawa na asilimia 23 ya watumiaji wote wa huduma za kifedha kwa njia ya simu nchini..
Airtel Money inachuana vikali na M Pesa na Tigo Pesa huku kampuni ya Vodacom inayomiliki M-Pesa ndiyo yenye sehemu kubwa ya soko la huduma za kifedha kwa njia ya simu kwa asilimia 39.

Latest