Agizo la Chalamila Stendi ya Magufuli laibua maoni mseto
- Wananchi wasema litasaidia kupunguza uhalifu.
- Uongozi wawataka wamiliki wa mabasi kutii sheria.
Dar es Salaam. Baadhi ya Wananchi wametoa maoni mseto kufuatia agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila, lililozitaka shughuli za mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani kuhamia katika Stendi Kuu ya mabasi ya Magufuli.
Agosti 11, 2026 Chalamila aliagiza mabasi yote yanayopakia abiria katika vituo vingine nje ya Stendi ya Magufuli iliyojengwa mwaka 2021 kuhamishia shughuli zao katika kituo hicho ili kiweze kutumika ipasavyo.
Uamuzi huo ulifikiwa baada ya uwepo wa makampuni ya mabasi yanayofanya shughuli zake bila kibali katikati ya miji, hali iliyopelekea msongamano katikati ya mji.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Nukta Habari baadhi ya wananchi wameunga mkono uamuzi huo wakieleza kuwa utasaidia kuimarisha usalama wa wasafiri.
“Wamefanya kitu ambacho ni kizuri sana, kwanza hata wahalifu wanaenda kule mjini moja kwa moja kulikuwa hakuna ukaguzi wowote na hapa mabasi yanaposhuka kuna vitengo vyote, kuna ukaguzi wa kila aina,” amesema Oscar Hava, mdau wa Stendi ya Magufuli.
Naye Miriam Kaniki mkazi wa Mbezi, amesema abiria wanapaswa kuheshimu miradi ya Serikali na kufuata utaratibu uliowekwa.
“Mradi wowote wa Serikali lazima uheshimiwe na wafanyabiashara, sisi kama abiria tunaona ni sawa tu, hatuwezi kukaidi kwa sababu hata Airport (kiwanja cha ndege) ipo moja tunaenda na hatuoni kama kuna umbali,” amesema.
Ni uamuzi wa ghafla
Wakati baadhi ya wasafiri na wafanyabiashara wakifurahia uamuzi wa kurudisha mabasi katiika kituo cha Magufuli, baadhi yao wamesema uamuzi huo umefanyika ghafla huku wengine wakihoji walioruhusu ujenzi wa vituo vingine vya mabasi nje ya Stendi ya Magufuli.
“Imekuwa ni ghafla kwa mwanzo, lakini ni wazo zuri kwa sababu kwanza litaipa heshima hii stendi kwa sababu ni kubwa na ina jina kubwa, tumelipokea vizuri, japo kwa mwanzo imetupa changamoto, amesema Glory Mbwambo
“Hawa waliojenga ofisi zilizoanzishwa nje ya (Kituo cha mabasi) Magufuli, wamenunua maeneo, wamepanga maeneo na wameona kuanzia mwanzo mpaka sasa wameendelea kununua kujenga lakini kwa nini wasiwakataze mwanzoni ni gharama kubwa, labda wangewapa muda sio ghafla,” amesema Deusdedith Mtiro.
Suala la mabasi kuhamia Stendi ya Magufuli iliyogharimu zaidi ya Sh50 bilioni limekuwa likisisitizwa na viongozi wa Serikali zaidi ya mara tatu, licha ya wamiliki wa mabasi kuendelea na shughuli zao katika vituo vingine.
Mwaka 2021, wakati Chalamila akiwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alitoa amri hiyo kwa mara ya kwanza baada ya wafanyabiashara kulalamika kukosa wateja kwa sababu ya mabasi kuikwepa stendi hiyo.
Mwaka mmoja baadae, aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Innocent Bashungwa alitoa agizo kama hilo Mei, 2022 ikifuatiwa na viongozi wengine pamoja na mamlaka ikiwemo Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) utekelezaji ukiwa hafifu.
Vibali ni vya kukata tiketi, si kupakia abiria
Akizungumzia suala hilo, Naamini Nguve, Meneja wa Stendi ya Magufuli, amsema ufuatiliaji wa vibali vya wamiliki wa vyombo vya usafiri haujaonesha kuwa kuna ruhusa ya kupakia abiria nje ya stendi kuu.
“Tumefuatilia vibali na hatujapata kibali chochote kinachoonesha kweli kuna watu ambao wameruhusiwa kufanya biashara katika maeneo nje ya Kituo cha Mabasi cha Magufuli, vibali walivyonavyo ni vibali ambavyo vinaonesha wameruhusiwa kukata tiketi na si kupakia abiria,” amesema Nguve.
Amesema hatua hiyo inapaswa kuangaliwa katika muktadha mpana wa mipango ya matumizi ya ardhi na usafiri katika jiji.
“Cha msingi ni watu wote waelewe kwamba mji wowote ule lazima uwe na mpango, mipango miji,” amesema.