Sababu, kukithiri kwa matukio ya vijana, watoto kujiua Tanzania
- Kila baada ya sekunde 40 mtu mmoja anajiua, sawa na takribani watu 1,974 kila siku, sababu kuu ikiwa ni uoga wa kujieleza
Dar es Salaam. Kila siku, mamia ya watoto huzaliwa duniani, wakianza safari mpya ya maisha yenye milima, mabonde, nyakati za furaha na huzuni.
Lakini nyuma ya safari hizi, kuna baadhi ya maisha yanayokatishwa ghafla kwa kujiua kabla hayajafikia kilele chake, ikichangiwa na sababu mbalimbali.
Shirika la Afya Duniani (WHO) linakadiria kuwa zaidi ya watu 720,000 hupoteza maisha kila mwaka kwa kujiua.
Hii ina maana kuwa kila baada ya sekunde 40 mtu mmoja anajiua, sawa na takribani watu 1,974 kila siku.

Nchini Tanzania, ripoti ya takwimu za mahabusu inayotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) inafafanua kuwa mwaka 2025 kulikuwa na jumla ya wafungwa 115 walioshukiwa kwa kosa la kuua au kujiua.
Idadi hiyo ni sawa na asilimia 0.6 ya wafungwa 19,646 waliokuwepo magerezani kufikia Desemba 2025.
Sababu zatajwa
Habari imezungmza na Dk. Paschal Kang’iria, Msaikolojia na Mratibu wa Afya ya Akili kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, amesema sababu kuu ya changamoto hiyo ni uoga wa kueleza changamoto wanazozipitia.
“Ni ngumu mtu kutafuta msaada kwa sababu anaona kama vile anawachosha watu katika mambo yake, mwishowe anaona ni jambo la aibu na kusema, ‘acha tu, nitaweza,” amesema Dk Paschal
Athari za mitandao ya kijamii
Kwa upande wake Moses Mmuya, mtaalamu wa afya ya akili kutoka ‘Buyegi Trust Fund Center’ Iringa, anaonya kuhusu athari za mitandao ya kijamii, hasa pale mtu anapoanza kupima thamani yake kwa mafanikio ya wengine au kwa idadi ya watu wanaovutiwa nae ama ‘koment’ anazopata.
“Mbona yule ametajirika, mbona mimi sijatajirika na tumesoma darasa moja? Kwa hiyo anajiona kwamba yeye ni mtu wa kushindwa.” amesema Mmuya.

Kwa watoto na vijana, changamoto inaweza kuwa kubwa zaidi kutokana na umri wao na maendeleo ya teknolojia. Mmuya anasema jamii inapaswa kuwa makini na maudhui yanayowafikia watoto kwa sababu wanaweza kuchukua kwa urahisi mambo wanayoyaona na kuyasikia.
Malezi na tamaduni hatarishi
Kwa mujibu wa Dk Kang’iria, malezi na tamaduni pia zinaweza kumfanya mtu anyamaze kuhusu matatizo anayopitia, hasa pale anapoamini kuwa kuzungumza ni kwenda kinyume cha mila au desturi.
“Kuna vitu ukivisema unaonekana kama wewe hufuati mila na desturi zinavyosema. Lakini kuna mambo si mazuri yanakuumiza, ila ukisema utaonekana umevunja mwiko,” Amesema.
Ukosefu wa taarifa sahihi
Aidha ameongezea kuwa, kuna baadhi ya watu hawana taarifa sahihi za wapi wanaweza kupata msaada ama wamfuate nani pindi wanapo kumbana na changamoto ya afya ya akili.
“Ukosefu wa taarifa sahihi kuhusu afya ya akili nao huchangia tatizo hilo, kwa kuwa taarifa zinaweza kubadilisha mitazamo ya watu na kuwafanya waone umuhimu wa kutafuta msaada,” Amesema Dk Paschal.
Unyanyapaa unazuia msaada
Mmuya anasema unyanyapaa bado ni kikwazo kikubwa kinachowafanya watu waogope kutafuta msaada.
“Jamii yetu imewajenga watu ambao wanaona hii changamoto ya afya ya akili kama udhaifu. Ukishaweka unyanyapaa kwenye jambo lolote lile, mtu hawezi kwenda kutafuta msaada.” amefafanua Daktari huuyo.

Anasisitiza kuwa changamoto za afya ya akili zinaweza kumpata mtu yeyote na kwamba jamii inapaswa kuongeza uelewa akiwarai wenye changamoto hiyo kuwahi katika vituo vya afya ili kupata msaada.
Dalili za kujiua zinazopaswa kutupiwa jicho
Dk Paschal anasema mabadiliko ya ghafla katika tabia ikiwemo kujitenga na marafiki, mahusiano kuyumba, kubadilika kwa namna ya kufikiri, kushuka kwa utendaji kazini au shuleni, matumizi makubwa ya pombe au dawa za kulevya, mabadiliko ya usingizi na hamu ya kula yanaweza kuwa dalili za mwanzo za kuiua
Mmuya anataja pia malezi yenye unyanyasaji na mateso wakati wa utoto kama mambo yanayoweza kuacha maumivu ya kihisia au trauma, ambayo yanaweza kuendelea kumuathiri mtu baadaye.
Migogoro ya kifamilia, changamoto za kifedha, matumizi ya dawa za kulevya na matarajio makubwa yasiyotimia pia yanaweza kuongeza msongo wa mawazo.