Matumizi ya intaneti Tanzania yapaa kwa asilimia 11.65
- Matumizi yamefikia petabyte 1,041 kutoka petabyte 932 kwa kipindi cha robo mwaka inayoishia Machi 2026.
Dar es Salaam. Matumizi ya intaneti nchini Tanzania yameongezeka kwa asilimia 11.65 katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita huku idadi ya usajili wa laini za intaneti ikiongezeka hadi milioni 62.79.
Takwimu za mawasiliano za robo ya mwaka inayoishia Juni 2026 iliyotolewa leo na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), inabainisha kuwa matumizi ya intaneti yamefikia petabyte 1,041 kutoka petabyte 932 kwa kipindi cha robo mwaka inayoishia Machi 2026.
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki aliyekuwa akiwasilisha ripoti hiyo leo Agosti 10,2026 amesema sekta ya mawasiliano imeendelea kukua na kuwa chachu ya uchumi na maendeleo nchini.
“Mwendendo huu unaonesha mabadiliko muhimu hususan katika maisha ya Watanzania kwenye simu na intaneti kwa sababu si tena dhana za mawasiliano pekee yake lakini zimekuwa ni miundombinu muhimu sana katika kuwezesha biashara, elimu, ajira, huduma za kifedha, upatikanaji wa taarifa, huduma za kijamii na mawasiliano kati ya wananchi na taasisi,” amesema Waziri.
Ukuaji wa matumizi ya intaneti unaendelea kuonyesha mabadiliko katika namna wananchi wanavyotumia teknolojia katika shughuli mbalimbali, ikiwemo biashara, huduma za kifedha, mawasiliano na upatikanaji wa taarifa.
Ripoti hiyo imeonesha kuwa pamoja na ukuaji wa matumizi ya intaneti, usajili wa laini za simu umefikia milioni 117, sawa na ongezeko la asilimia 4.51 ikilinganishwa na robo ya Machi 2026.
Aidha, idadi ya simu janja imeongezeka kwa asilimia 5.16 na kufikia milioni 31.34, hali inayoendana na kuongezeka kwa matumizi ya huduma za intaneti kupitia vifaa vya kidijitali.
TCRA imesema mwenendo huo unaashiria kuendelea kuimarika kwa upatikanaji wa huduma za mawasiliano nchini pamoja na kuongezeka kwa matumizi ya huduma zinazotolewa kwa njia ya kidijitali.