Rais Samia azindua tume kuchunguza wahusika wa ghasia za Oktoba 29,2025
- Tume hiyo itaongozwa na Jaji Mstaafu Shaban Lila, yapewa siku 150 kukamilisha uchunguzi.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amezindua Tume ya Rais ya Uchunguzi wa Wahusika wa Ghasia na Ukiukaji wa Sheria katika matukio ya ghasia yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, akisisitiza kuwa tume hiyo inapaswa kutekeleza jukumu lake kwa weledi, uadilifu na bila kuingiliwa ili kubaini ukweli kuhusu matukio hayo.
Tume hiyo yenye wajumbe sita imezinduliwa leo, Agosti 7, 2026, jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mapendekezo ya Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya kabla na baada ya uchaguzi mkuu.
Uzinduzi huu unakuja ikiwa zimepita siku 106 baada ya kuwasilishwa kwa ripoti ya Tume ya Jaji Chande Aprili 23, 2026 na siku 262 tangu hatua ya kuanzishwa kwa mchakato wa kuundwa tume ya uchunguzi Novemba 18, 2025.
Hii inakuwa tume ya pili kushughulikia matukio yaliyotokea katika kipindi cha uchaguzi wa Oktoba 29, 2025, licha ya kukosolewa vikali na baadhi ya asasi za kutetea haki za binadamu pamoja na vyama vya upinzani, ikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Rais Samia aliyekuwa akizingumza wakati uzinduzi huo amesema ana imani wajumbe walioteuliwa watatumia taaluma, uzoefu na viapo vyao vya kazi kutekeleza jukumu hilo kwa haki na ufanisi.
“Ni imani yangu kwamba majaji hawa watatumia taaluma, uzoefu na viapo vyao kutekeleza kazi hii kwa weledi, umakini na uadilifu mkubwa. Endapo kutakuwa na ulazima wa kuongeza muda, tutalifanyia kazi jambo hilo,” amesema Rais Samia.
Tume hiyo imepewa muda wa siku 150 kukamilisha uchunguzi wake na kuwasilisha ripoti ya utekelezaji wa majukumu yake ikitarajiwa kutoa majibu juu ya waliohusika kuratibu ghasia hizo zilizochafua taswira ya Tanzania.
Tume hiyo itaongozwa na Jaji Mstaafu Shaban Ali Lila kama Mwenyekiti, huku wajumbe wengine wakiwa Jaji Petrus Tilainge Damas kutoka Namibia, Jaji Barishaki Cheborion kutoka Uganda, pamoja na Jaji Mstaafu Godemas, Jaji Mstaafu Awadh Mohammed Bawazir na Jaji Mstaafu Aishieli Nelson Sumari kutoka Tanzania.