Brussels kufungua milango ya utalii, safari za ndege Tanzania
- Ni baada ya kutua Tanzania tangu kusainiwa kwa mkataba Novemba 3, 2021
Dar es Salaam. Hatimaye baada ya miaka mitano Shirika la Ndege la Brussels kutoka nchini Ubelgiji limeanza safari zake rasmi moja kwa moja kutoka nchini humo kuja Tanzania.
Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Tanzania mkataba kuhusu kutua kwa ndege hiyo katika ardhi ya Tanzania ulisainiwa Novemba 3, 2021 jijini Dodoma, ukilenga kuimarisha ushirikiano katika sekta ya usafiri wa anga, biashara, utalii na uwekezaji.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, James Millya aliyekuwa akizungumza wakati wa mapokezi ya ndege hiyo iliyowasili kwa mara ya kwanza ikiwa na watalii 248 Juni 3, 2026 alisema ndege hiyo itakuwa ikifanya safari zake moja kwa moja kutoka nchini Ubeligiji kuja Tanzania kupitia uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).
Huenda ujio wa ndege hiyo kutoka Shirikala la Brussels linalohudumia zaidi ya vituo 90 duniani, likafungua fursa mpya za kiuchumi na kuongeza idadi ya watalii wataoingia Tanzania ambao kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu mpaka kufikia Machi 2026 jumla ya watalii 4,086 waingia Tanzania kutokea nchini Ubelgiji
Mbali na kuongeza idadi ya watalii, huenda Brussels ikarahisisha safari za moja kwa moja kuelekea bara la Ulaya na kuondoa usumbufu kwa watanzania ambapo awali walilazimika kuunganisha safari za ndege kupitia nchi zaidi moja.
Kuja kwa ndege ya Brussels kunakuja kuongeza idadi ya safari za ndege za moja kwa moja kutoka Tanzania kwenda nje ya Afrika ambazo kwa sasa zilizo nyingi hutegemea na ratiba za ndege za mashirika husika.
Kwa sasa watanzania wanaweza kusafiri kwenda moja kwa moja kutoka Tanzania kwenda Bara la Ulaya, Mashariki ya Kati na Bara la Asia huku safari ndefu zaidi ikifanywa na Shirika la Ndege la Air Tanzania kuelekea Guangzhou nchini China.
Hata hivyo, hivi karibuni Air Tanzania ilitangaza kuanza safari za ndege moja kwa moja kutoka Tanzania kwenda London ifikapo Julai 2027 safari inayotajwa kuwa ni safari ndefu zaidi ya shirika hilo tangu kufufuliwa kwake upya mwaka 2016.