Rais Samia aunda tume ya uchunguzi wa makosa ya kijinai ya Oktoba 29
- Tume hiyo inaundwa wiki tatu tangu tume ya Jaji Chande iwasilishe ripoti yake kwa Rais Samia.
Arusha. Rais Samia Suluhu Hassan ameunda tume ya uchunguzi wa kijinai ya matukio ya ghasia ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 itakayoongozwa na Jaji Shabani Ally Lila.
Taarifa ya Katibu Mkuu Kiongozi Dk Moses Kusiluka, iliyotolewa leo Mei 18, 2026 imebainisha kuwa uamuzi huo umetokana na mapendekezo ya Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani Yaliyotokea Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025 na kwa kuzingatia mamlaka ya Rais chini ya Sheria ya Tume za Uchunguzi, Sura ya 32.
Tume hiyo inaundwa baada ya takribani wiki tatu tangu tume ya kuchunguza matukio ya vurugu za wakati na baada ya uchaguzi mkuu maarufu kama tume ya Jaji Chande iwasilishe ripoti yake mbele ya Rais Samia ikibainisha mapendekezo yaliyolenga kuponya Taifa baada ya kupitia kipindi hicho cha ghasia.
Hata baada ya kuwasilisha ripoti hiyo iliyochukua siku 153 kukamilika, tume hiyo iliendelea kosolewa vikali na watetezi wa haki za binadamu na vyama vikuu vya upinzani ikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Watatu wateuliwa
Mbali na Jaji Shabani, taarifa ya Kusiluka imeeleza kuwa Rais Samia Suluhu Hassan amewateua pia majaji wastaafu watatu wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambao ni Gad John Mjemmas, Awadh Mohammed Bawazir na Aishieli Nelson Sumari.
Aidha, Taarifa hiyo haijabainisha lini wateule hao wataapishwa rasmi kwa ajili ya kuanza kazi.
Latest