Soko la fedha za kigeni laonyesha utulivu, Dola ya Marekani yabaki Sh2,650
Dar es Salaam. Viwango vya kubadilisha fedha za kigeni dhidi ya Shilingi ya Tanzania vimeendelea kuonyesha utulivu katika wiki ya mwisho ya Aprili, huku baadhi ya sarafu zikibaki katika viwango vilevile vilivyorekodiwa wiki iliyopita.
Kwa mujibu wa viwango vya kubadilisha fedha za kigeni vilivyotolewa na Benki za NMB na CRDB leo Aprili 27,2026 Dola ya Marekani (USD) imeendelea kununuliwa kwa Sh2,570 na kuuzwa kwa Sh2,650 ikiwa ni sawa na kiwango kilichorekodiwa wiki iliyopita.
Hata hivyo, uchambuzi wa mwenendo wa viwango hivyo ndani mwezi mmoja kuanzia Machi 27 unaonesha kuimarika kwa Dola ya Marekani kutoka Sh2,635 iliyotumika kuuza sarafu hiyo na kununuliwa kwa Sh2,555 katika benki zote mbili.
Sarafu nyingine ikiwemo Euro zimeonesha mabadiliko kidogo ikishuka katika Benki ya CRDB kutoka Sh2,931.77 (kununua) hadi Sh2,899.8, na kutoka Sh3,231.77 (kuuza) hadi Sh3,199.8 kulinganisha jumatatu iliyopita Aprili 20, 2026.

Hali kama hiyo imeonekana pia kwa Rand ya Afrika Kusini (ZAR) na Rupia ya India (INR) ambazo zimepungua kwa viwango vidogo.
Kwa upande mwingine, baadhi ya sarafu katika Benki ya NMB zimeendelea kubaki karibu na viwango vya awali, zikionyesha mabadiliko yasiyo makubwa yenye kuashiria soko lenye utulivu.
Utulivu huu wa viwango unaashiria uwiano kati ya mahitaji na upatikanaji wa fedha za kigeni nchini, hali inayoweza kusaidia kudhibiti mfumuko wa bei, hasa kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje.
Kwa wafanyabiashara wanaoagiza bidhaa nje ya nchi, kutokuwepo kwa mabadiliko makubwa kunarahisisha upangaji wa gharama na kupunguza hatari ya kupanda kwa bei ghafla. Aidha, wawekezaji hupata mazingira yenye uhakika zaidi wa kufanya maamuzi ya kifedha.
Kwa upande wa Serikali, mwenendo huu unaweza kuashiria uimara wa sera za fedha na usimamizi mzuri wa akiba ya fedha za kigeni, ingawa hali hii inaweza kubadilika kulingana na mwenendo wa soko la dunia, hususan thamani ya dola ya Marekani.
Latest