Dk Mwigulu Nchemba Waziri Mkuu mpya Tanzania
- Mwigulu anakuwa Waziri Mkuu wa 10 akiongoza Serikali kwa miaka mitano ijayo.
Arusha. Rais Samia Suluhu Hassan amemteua Dk Mwigulu Nchemba kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
Jina la Dk Mwigulu Nchemba kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania limewasilishwa Bungeni Dodoma leo Novemba 13, 2025 na Mpambe wa Rais (ADC) Brigedia Jenerali Nyamburi Mashauri na kusomwa na Spika wa Bunge Mussa Azzan Zungu.
“Kwa kutekeleza matakwa ya kikatiba nimemteua Mheshimiwa Dk Mwigulu Lameck Nchemba kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania,” amesema Spika Zungu akinukuu barua ya Rais Samia iliyosomwa Bungeni ikifuatiwa na shangwe kutoka kwa wabunge wengine wakimpongeza Dk Nchemba.
Mwigulu ambaye pia amewahi kuwa Waziri wa Fedha kwa awamu mbili zilizopita anakuwa Waziri Mkuu wa 10 akichukua nafasi ya Kassim Majaliwa aliyehudumu nafasi hiyo kwa miaka 10 iliyopita chini ya Rais wa awamu ya tano John Pombe Magufuli na baadae Rais Samia Suluhu baada ya mtangulizi wake kupoteza maisha.
Kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania Waziri Mkuu wa Tanzania huchaguliwa na Rais anayeingia madarakani ndani ya siku 14 tangu kutangazwa kwa matokeo ya urais.
Kiongozi huyo wa juu zaidi Serikalini anapaswa kuwa mbunge wa kuchaguliwa kutoka katika jimbo la uchaguzi katika chama cha saisa chenye wabunge wengi ndani ya siku 14 baada ya kushika madaraka hayo.
Ikiwa hakuna chama cha siasa chenye wabunge wengi atakayechaguliwa ni yule anayeeleeka kuungwa mkono na wabunge wengi kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania.
Baada ya uteuzi huo, Bunge la Tanzania lilimthibitisha Nchemba kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania kwa kura 369 kati ya kura 371 ambapo kura mbili ziliharibika.
Akizungumza baada ya uthibitisho huo Mwigulu ameahidi kufanya kazi yake kwa uadilifu bila upendeleo kwa wabunge wote huku akikidhi matarajio ya Watanzania.
“Natambua uzito wa majukumu yangu (ya Uwaziri Mkuu) pamoja na matarajio yake, pamoja na matarajio ya Watanzania. Nitafanya kazi kwa bidii na uaminifu kwa jitihada kubwa kuweza kukidhi matarajio hayo,” amesema Nchemba ambaye pia ni mbunge wa Iramba Magharibi..
Kwa mujibu wa taarifa ya Katibu Mkuu wa Serikali Dk Moses Kusiluka iliyotolewa leo November 13, 2025 Dk Mwigulu ataapishwa na Rais Samia Suluhu Hassan kesho Novemba 14, 2025, Chamwino Dodoma saa 4 asubuhi.
Latest