Rais Samia kuchaguliwa Uenyekiti Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC

August 15, 2024 11:36 am · Fatuma Hussein
Share
Tweet
Copy Link
  • Atarithi nafasi ya Hakainde Hichilema anayemaliza muda wake.
  • Ni katika Mkutano wa 44 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa (SADC)

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajia kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika SADC akipokea kutoka kwa Rais wa Zambia Hakainde Hichilema anayemaliza muda wake.

Jukumu kubwa la asasi hiyo ni kuangalia masuala yote yanahusiana na Siasa, ulinzi na usalama katika ukanda wa SADC huku changamoto kubwa kwa sasa ikiwa ni namna ya kutafuta suluhu ya kudumu hususani katika eneo la Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo-DRC.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu Rais Samia atachaguliwa kushika nafasi hiyo katika Mkutano wa 44 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa (SADC) utakaofanyika Agosti 17,2024 mjini Harare nchini Zimbabwe.

Utaratibu wa kuwa Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi, na Usalama ya SADC unafuata mzunguko wa uongozi kati ya nchi wanachama.

Uongozi wa asasi hii huhamishwa kutoka kwa kiongozi mmoja kwenda kwa mwingine kutoka nchi tofauti ili kuhakikisha usawa wa uwakilishi na ushiriki wa nchi wanachama wote katika kusimamia masuala ya siasa na usalama.

Aidha, kwa mujibu wa taarifa hiyo Rais Samia anatarajia kuondoka nchini leo Agosti 15, 2024 kuhudhuria mkutano huo wenye kauli mbinu ya kukuza ubunifu ili kufungua fursa za ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu kuelekea SADC yenye viwanda.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW