Jaji mstaafu Othman ateuliwa kuwa mkuu wa chuo Ardhi
- Aliwahi kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania
- Pia Rais Samia amemteua Profesa Elisante Ole Gabriel kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluh Hassan amefanya uteuzi wa viongozi mbalimbali akiwemo Jaji Mkuu mstaafu Mohamed Chande Othman ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ardhi (ARU).
Jaji Othman amechukua nafasi iliyoachwa na Waziri Mkuu wa zamani na Makamu wa Rais wa Tanzania, Cleopa Msuya.
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu Jaffar Haniu katika taarifa yake iliyotolewa leo Agosti 17, 2021 amesema Rais Samia pia amemteua Profesa Elisante Ole Gabriel kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.
Kabla ya uteuzi huu Profesa Ole Gabriel alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi upande wa mifugo. Profesa Ole Gabriel anachukua nafasi ya Mathias Kabunduguru ambaye amestaafu.
Profesa Ole Gabriel ataapishwa Agosti 21, 2021 Ikulu Jijini Dar es Salaam pamoja na mabalozi wateule watatu ambao ni Balozi mteule Luteni Jenerali Yakub Hassan Mohamed aliyeteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania Nchini Uturuki.
Balozi mteule Mahmoud Thabit Kombo aliyeteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia na Balozi Mteule Elsie Sia Kanza aliyeteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Marekani.
Latest
