Shirika la ndege la Emirates lawekeza Sh310.5 bilioni kuwaburudisha wateja wake kwa “wine”

August 27, 2019 2:54 pm · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link
  • Hivi karibuni, shirika hilo liliwaonjesha wadau wake mvinyo wa aina tofauti ili kupata mvinyo bora utakaotumika kwenye ndege zake.
  • Imewekeza kiasi hicho kwenye mvinyo na pombe kali aina ya “spirit” ambazo zitatumika kwenye ndege zake hasa daraja la kwanza na la biashara.
  • Kampuni za Tanzania zatakiwa kuchangamkia fursa ya kuliuzia shirika hilo mvinyo unaotengenezwa nchini. 

Dar es Salaam. Katika kudumisha uhusiano na wateja wake, mashirika ya ndege hutumia vivutio mbalimbali kuwaburudisha wateja wanapokuwa safarini.

Vivutio hivyo ni pamoja na chakula na vinywaji kama mvinyo (Wine) ambao hutumiwa katika safari za masafa marefu.

Hivi karibuni, shirika la ndege la Emirates liliandaa tukio kwa ajili ya kuwaonjesha wadau wake mvinyo wa aina tofauti ili kupata mvinyo bora utakaotumika kwenye ndege zake, licha ya kuwa wamekuwa wakitoa huduma hiyo kwa muda mrefu. 

Taarifa iliyotolewa na shirika hilo, zaidi ya Dola za Marekani milioni 135 (takriban Sh310.5 bilioni) zimetumika katika kuwekeza kwenye mvinyo na pombe kali aina ya “spirit” ambazo zitatumika kwenye ndege za Emirates kwenye daraja la kwanza na la biashara.

“Emirates imefanya uwekezaji huu mwaka jana ikifanya kazi moja kwa moja na watengenezaji wa vinywaji vikali na mvinyo ulimwenguni kote,” amesema Hendrik du Preez ambaye ni Meneja wa kampuni ya Emirates ukanda wa Africa Mashariki.

Kwa mujibu wa takwimu za shirika hilo, chupa milioni 2.3 za mvinyo na “champaigne” hutumika kwenye daraja la kwanza na la biashara kwenye ndege zake huku zaidi ya chupa milioni 3 zikitumika kwenye daraja la uchumi kila mwaka.

Emirates imesema ina timu ambayo imejenga mahusiano na wabobezi wa kutengeneza mvinyo kote ulimwenguni nao huchagua bidhaa bora ambazo zitawafurahisha wateja wake.

Kwa sasa, Emirates imechagua mvinyo kutoka mataifa mbalimbali ikiwemo Afrika Kusini na Ufaransa amabazo baadhi yake zimekuwa zikitumika na shirika hilo tangu mwaka 2007.

baadhi ya mvinyo na “champaigne” zilizoonyeshwa kwenye hafla ya Emirates. Picha| Emirates

Licha ya kuwa Tanzania inazalisha zabibu hasa katika mkoa wa Dodoma na ina viwanda vya mvinyo, haiko miongoni mwa nchi zinazotoa mvinyo unaotumika kwenye ndege za Emirates.

Hiyo ni fursa nyingine kwa kampuni za Tanzania zinazotengeneza mvinyo kuzipigia chepuo bidhaa zake zitumike kwenye ndege za kimataifa ambazo zinafanya safari nchini.


Zinazohusiana:


Hata hivyo, baadhi ya wadau wa usafiri wa anga wamesema wazalishaji wa mvinyo na bidhaa zingine nchini bado hawana matangazo ya kutosha ambayo yanaweza kufanya mashirika ya ndege  yawatambue.

Mathias Kitula ambaye ni mfanyabiashara ambaye husafiri mara kwa mara akitumia ndege za Emirates kwenda Dubai, amesema anapokuwa kwenye ndege hutumia vinywaji hasa vya Afrika Kusini na vingine vya mataifa ya Magharibi.

“Hamna matangazo ya kuonyesha kuwa nao wanazalisha. Cha msingi watengeneze matangazo mazuri ili bidhaa zetu ziende kwenye ngazi ya kimataifa,” amesema Kitula.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW