Corona: Masharti mapya kuingia bungeni Dodoma
- Watakaoruhusiwa ni wale wenye shughuli za kiofisi tu.
- Hiyo ni tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Uviko-19.
Dar es Salaam. Wakati vikao vya kamati 14 za kudumu za bunge zikianza jijini Dodoma leo, Ofisi ya Bunge imesema wanaoruhusiwa kuingia bungeni ni wageni wanaofika kwa shughuli za kiofisi ili kuepusha mkusanyiko wa watu na maambukizi ya Uviko-19.
Taarifa iliyotolewa na uongozi wa bunge Agosti 17, 2021 imesema kuwa kulingana na uwepo wa maambukizi ya corona nchini watakaoruhusiwa kuingia bungeni ni waandishi wa habari waliosajiliwa kwa ajili ya kutoa habari za bunge.
Wengine ni wadau watakaohudhuria vikao vya kamati kwa ajili ya kutoa maoni ambao wataelekezwa na kamati inayohusika kabla ya kikao cha kupokea maoni.
“Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imekuwa ikitoa elimu na miongozo mbalimbali ya kujikinga pamoja na kuchukua hatua katika kuthibiti kuenea kwa maambukizi ya virusi vya corona,
“Hivyo imetoa tahadhari katika vikao vya kamati 14 za kudumu za bunge zinazokutana t18 – 29 Agosti, 2021 kwa sababu vikao hivyo vinahusisha mkusanyiko wa waheshimiwa wabunge, watumishi wa Bunge, watendaji wa Serikali, waandishi wa wabari na wageni wengine mbalimbali,” imeeleza taarifa hiyo.
Aidha katika kutekeleza kwa vitendo tahadhari hizo za kiafya uongozi wa bunge umeweka utaratibu wa uendeshaji wa vikao vya kamati ambao ni kutumika kwa kumbi kubwa saba kwa ajili ya vikao vya kamati.
Pia kamati zitakutana kwa kupishana yaani kamati saba ni kuanzia saa 3:00 asubuhi – saa 7:30 mchana na kamati nyingine saba kuanzia saa 8:00 mchana mpaka saa 12:30 jioni.
Pia kila kamati itafanya vikao kwa namna inayozingatia muda uliopangwa ili kutoathiri muda wa kuanza kwa vikao vya kamati nyingine na idadi ya watendaji wanaokuja na waziri kwenye vikao isizidi maafisa watano wa wizara kwa kila kikao.
Latest