Ukosefu wa ajira, mahitaji ya familia: Sababu watu kuchagua ajira zisizo rasmi Dar
- Asilimia 58 ya kaya zote mkoani humo zinategemea kipato katika sekta hiyo.Â
- Kuongezeka kwa mahitaji ya familia kwachangia.
- Wanawake waingia mzigoni kuwasaidia wanaume.
Dar es Salaam. Ni jambo zuri ya kuwa siyo Watanzania wote wanasubiri ajira za kuajiriwa.Â
Elimu ya ujasiriamali na kujiajiri imeshika kasi miongoni mwa Watanzania na kuwafanya kuwekeza muda wao kutafuta fursa za kujiajiri ili kuboresha maisha yao.
Mathalan, katika Jiji la Dar es Salaam, kaya 767,904 sawa na asilimia 58 ya kaya zote (1.3 milioni) mkoanii humo zinategemea kipato kinachotokana na sekta isiyo rasmi.
Hiyo ikiwa ni kwa mujibu wa Ripoti ya utafiti wa sekta zisizo rasmi ya mwaka 2019 iliyotolewa na Ofisi ya taifa ya Takwimu (NBS).
Hiyo ina maana kuwa kwa kila kaya 10 basi takriban sita zinategemea kipato kinachotokana na sekta isiyo rasmi jijini humo.
Katika sekta hiyo isiyo rasmi wakazi hao wanajishughulisha na ujenzi, kilimo, malazi na huduma za chakula, uzalishaji, ufundi stadi, uuzaji wa bidhaa za jumla, uvuvi na utunzaji misitu.
Zipo sababu mbalimbali zilizochangia wakazi wa jiji hilo kuingia katika sekta isiyo rasmi ikiwemo kupata kipato cha kukijikiku ngazi ya familia.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa, asilimia 55.2 ya wakazi wa Dar es Salaam wanaojihusisha na ajira zisizo rasmi wanafanya shughuli hizo kwa sababu wamekosa ajira zingine (rasmi).
Pia asilimia 55.1 ya wanake wamesema kukosa kazi rasmi kunawafanya kuingia katika ajira zisizo rasmi.
Sababu nyingine ni famiia kuhitaji kipato cha ziada. NBS imeeleza kuwa, asilimia asilimia 54.3 ya wakazi wa Dar es Salaam wanaojihusisha na ajira zisizo rasmi wana changamoto za kipato hivyo kuwalazimisha wanafamilia kutafuta njia mbadala za kupata kipato.
Sababu hii imetolewa na wanawake wengi zaidi (asilimia 58.4) hivyo kuashiria kuwa kipato cha wanaume hakikidhi mahitaji ya familia na hivyo wanawake kulazimika kuingia mtaani kusaka pesa.