CAG: Dawasa ilikusanya mamilioni bila kusoma mita za maji
- Sh755.65 milioni zilikusanywa na mamlaka hiyo
- CAG asema hali hiyo inaweza kuifanya Dawasa kubambikiza ankara au kukusanya mapato pungufu.
- Mifumo ya kiteknolojia ya ulipaji ankara za maji yaanzishwa kumaliza tatizo hilo.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) imekuwa ni moja kati ya mamlaka zilizoanikwa mapungufu yake na Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya mwaka 2020/21 kutokana na udhaifu katika usomaji mita za maji.
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Charles Kichere amemweleza Rais Samia Suluhu Hassan leo Machi 30 jijini Dodoma kuwa Dawasa ilitoza bili za maji kwa wateja 1,207 na kukusanya Sh755.65 milioni bila kusoma mita za maji kwa matumizi ya maji ya kila mwezi.
Kati ya idadi hiyo wateja 371 walikuwa na mita mbovu huku 836 wakitozwa huduma za maji taka bila kuwa na taarifa sahihi zinazotumika kukadiria gharama za maji taka.
“Utaratibu huu Mheshimiwa Rais unaweza kusababisha wateja kulipa zaidi au pungufu ya kiasi kilichotakiwa,” amesema Kichere.
Wateja wa Dawasa kwa nyakati tofauti wamekuwa wakilalamikia uwepo wa ankara za maji zisizokuwa na uhalisia.
Zinazohusiana:
-
CAG katika namba: Matumizi, mapato ya Air Tanzania juu
-
Ripoti ya CAG katika namba
-
CAG abaini taasisi tisa zilizofanya malipo ya mamilioni bila kuidhinishwa
Katika kutatua changamoto hiyo, Rais Samia Suluhu amesema kuwa kuna mifumo mipya ya kiteknolojia ya ulipaji bili za maji imeanzishwa ili kuboresha huduma za ulipaji wa bili hizo.
Mifumo hiyo, Rais Samia amesema itamuunganisha mteja moja kwa moja na zitamuwezesha kuhakikisha kama bili atakayotumiwaa ni sahihi au la.
“ Siku ya maji tuliyoifanya 22 mwezi huu (Machi) kuna systems (mifumo) mpya zimeanzishwa kuna Maji App lakini kuna ‘unified water bills’ (Mjumuisho wa bili za maji) ambako sasa bili sasa zitatoka kwa kutumia Tehama na sidhani kama kutakuwa na human control au kupeleka bili ambazo mita hazikusomwa,” Rais Samia.
Latest