Bei za petroli, dizeli hazishikiki Tanzania

August 3, 2022 7:09 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Bei za mafuta zimepanda tena mwezi Agosti kwa viwango tofauti.
  • Sababu kubwa ni kupanda kwa bei katika soko la dunia.
  • Serikali yatoa Sh100 bilioni kupunguza makali.

Dar es Salaam. Bei ya mafuta imeendelea kupanda kwa kiwango cha juu Agosti nchini Tanzania huku sababu kubwa ya upandaji wa mafuta huo ni kuendelea kuongezeka kwa bei ya nishati hiyo duniani.

Bei mpya za rejareja zilizotangazwa Agosti 2, 2022 na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), bei ya petroli inayopitia bandari ya Dar es Salaam imepanda hadi kufikia Sh3,410 kwa lita moja, dizeli Sh3,322 na mafuta ya taa 3,765.

Ongezeko hilo la bei ya petroli ni sawa na asilimia 5.9 ya bei iliyotumika mwezi Julai, dizeli asilimia 5.6 na mafuta ya taa asilimia 9.3 

Kwa bei hizo, itawafanya wamiliki wa vyombo vya moto jijini hapa kutoboa zaidi mifuko yao ukilinganisha na mwezi Julai ambapo kwa Sh10,000 waliweza kupata lita 3.1 sasa kwa pesa hiyo wanaweza kupata lita 2.9 tu.

Bei hizo ni baada ya Serikali kutoa ruzuku ya Sh100 bilioni kwa ajili ya kupunguza makali ya bei ya nishati hiyo.

Hata wakati bei hiyo  ikipanda kwa mafuta yanayoingilia  bandari ya Dar es Salaam, bei za mafuta kwa bandari ya Tanga na Mtwara nazo zimepanda ukilinganisha na zile za mwezi Julai

Kwa wamiliki wa vyombo vya moto wanaotumia mafuta yanayopitia Bandari ya Tanga nao watapata maumivu kwa sababu bei iko juu ikilinganishwa na bandari zingine. Mafuta hayo hutumiwa zaidi na wananchi wa mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara.

Bei ya petroli yanayopitia katika bandari hiyo kwa Agosti inauzwa Sh3,435 kwa lita ikiwa imepanda kutoka Sh3,214 ya mwezi uliopita. Dizeli imefikia  Sh3,349 ukilinganisha na 3,150 iliyotumika mwezi Julai.

Kwa mafuta yanayopitia Bandari ya Mtwara, bei ya petroli imefikia  Sh3,393, sawa na ongezeko la Sh188 huku dizeli ikiongezeka kwa Sh179 na kufikia Sh3,351 kwa mwezi Agosti.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW