Zaidi ya Sh191 milioni kupambana na polio Mwanza

August 31, 2022 5:19 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Zitatumika katika zoezi la kutoa chanjo hiyo kwa watoto 115,815.

Mwanza. Zaidi ya watoto 115,815 wanatarajiwa kupewa chanjo ya polio awamu ya tatu katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza ili kuwakinga na ugonjwa huo ambao usipodhibitiwa unaweza kusababisha kupooza.

Katika kampeni hiyo ya awamu ya tatu zaidi ya Sh191.6 milioni zinatarajiwa kutumika ikiwa ni pamoja na kusambaza chanjo kwenye maeneo ya kutolea chanjo hiyo, kutoa mafunzo kwa watoa huduma za afya ngazi ya halmashauri, kutoa mafunzo kwa wenyeviti wa mitaa na kutoa taarifa kwa watendaji wa kata.

Akizungumza kwenye kikao cha Kamati ya Kudumu ya Afya Ngazi ya Jamii Agost 30,2022, Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi amewataka wenyeviti wa mitaa kutoa ushirikino ili kuweza kuwafikia watoto wote ambao hawakufikiwa na huduma hiyo awamu ya pili.

“Tulifanya vizuri kwenye utoaji wa chanjo hiyo awamu ya pili ambapo lengo tulijiwekea kuchanja watoto 94,000 lakini tulivuka lengo na kufanikiwa kuchanja zaidi ya watoto 100,000 sawa na asilimia 116,” amesema Makilagi.

Mkuu huyo wa wilaya anaamini kwa kutumia mbinu na njia zile zile za awamu ya pili, malengo waliyojiwekea awamu ya tatu ya kuchanja watoto 115,815 yatafikiwa  kupitia vituo vilivypendekezwa ikiwemo nyumba za ibada, masokoni, na vituo vya afya.

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya jiji la Mwanza, Sebasitian Pima amesema zoezi hili litaanza kufanyika kuanzia Septemba 1 hadi 4 mwaka huu na kuomba wananchi kutoa ushirikiano ili kuweza kuwapatia kinga watoto ambao hawakufikia katika awamu iliyopita.

Enable Notifications OK No thanks