Arusha yaongoza uzalishaji maziwa ya ng’ombe Tanzania
Uzalishaji wa maziwa ni kazi ya kiuchumi ambayo imekuwa ikiwapatia wafugaji kipato kwa ajili ya kuendesha familia. Picha TADB.
- Umezalisha asilimia 8.1 ya maziwa yote ya Tanzania Bara.
- Uzalishaji wa maziwa nao waongezeka kwa asilimia 24.5 kwa miaka 12.
- Teknolojia ya kisasa na unywaji utachochea soko la maziwa ya Tanzania ndani na kimataifa.
Dar es Salaam. Wakati uzalishaji wa maziwa ya ng’ombe ukiongezeka kwa asilimia 24.5 katika kipindi cha miaka 12 nchini Tanzania, Mkoa wa Arusha ndiyo kinara wa uzalishaji zao hilo ambalo hutumika katika shughuli mbalimbali ikiwemo usindikaji viwandani.
Ripoti ya Sensa ya Taifa ya Kilimo kwa mwaka 2019/20 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) inaeleza kuwa uzalishaji wa maziwa umeongezeka hadi lita bilioni 3.1 mwaka 2019/20 kutoka lita bilioni 2.5 mwaka 2007/08.
Hiyo ni sawa na ongezeko la asilimia 24.5 katika kipindi cha miaka 12.
Kati ya kiasi hicho cha maziwa kilichopatikana, asilimia 95.5 kilizalishwa na wafugaji wadogo ambao wengi wao hufuga kienyeji katika nyumba zao au mashambani.
Kwa ng’ombe wanaofugwa kienyeji walikuwa wanazalisha wastani lita tatu kwa siku huku ng’ombe wanaofugwa kisasa walikuwa na uwezo wa kutoa wastani wa lita saba mpaka tisa za maziwa.
“Kuongezeka kwa maziwa ya ng’ombe kumechangiwa na utekelezaji wa sera ambayo inalenga kutumia rasilimali zilizopo kwa ufugaji ng’ombe wa kibiashara ili kuongeza kipato kwa wafugaji na kuboresha maisha yao,” imeeleza ripoti hiyo.
Mikoa 10 inayoongoza kwa uzalishaji wa maziwa
Licha ya wazalishaji wa maziwa kukabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu teknolojia, Mkoa wa Arusha ndiyo umetajwa kuongoza kwa uzalishaji wa maziwa mengi Tanzania Bara.
Mwaka 2019/20, mkoa huo ulizalisha lita milioni 247.9 sawa na asilimia 8.1 ya maziwa yote yaliyozalishwa, ukifuatiwa na Dodoma na Tabora,
Mkoa wa Mtwara ndiyo ulikuwa na uzalishaji wa chini kabisa Tanzania Bara wa lita milioni 5.8.
Licha ya Mtwara kushika nafasi ya mwisho katika uzalishaji wa zao hilo lakini ndiyo mkoa ambao bei ya maziwa ilikuwa juu kuliko maeneo mengine, ikidhihirisha uhitaji wa maziwa mkoani humo ulikuwa mkubwa.
Ripoti hiyo ya Sensa ya Taifa ya Kilimo ya 2019/20 inaeleza kuwa lita moja ya maziwa ilikuwa inauzwa Sh2,000 ikifuatiwa na Dar es Salaam kwa Sh1,665.
Bei ya chini ya maziwa kwa wakati huo ilirekodiwa mkoani Katavi kwa Sh539 kwa lita moja katika kipindi cha mvua huku Sh790 ilirekodiwa katika Mkoa wa Tabora katika kipindi cha ukame.
Licha ya kuongezeka kwa uzalishaji wa maziwa nchini, bado uagizaji wa maziwa na bidhaa zake nje ya nchi uko juu, hivyo juhudi zinahitajika kuongeza uchakataji wa maziwa ya ndani ili kuongeza matumizi ya zao hilo na bidhaa zake.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki katika hotuba ya bajeti ya mwaka huu alisema katika kipindi cha mwaka 2021/22 Wizara kupitia Bodi ya Maziwa Tanzania itaanzisha programu ya mashamba ya kibiashara ya ufugaji wa ng’ombe wa maziwa (Small Scale dairy farms) na programu ya majaribio ya unywaji wa maziwa shuleni.
“Tutajenga vituo vya ukusanyaji maziwa 25; na kuendelea kuimarisha udhibiti wa uingizwaji holela wa maziwa kutoka nje ya nchi,” alisema Ndaki ikiwa ni hatua ya kuongeza uzalishaji na matumizi ya maziwa yanayozalishwa Tanzania.
Latest