Salamu za Dk Gwajima kwa wasiosajili vituo vya kulelea watoto
- Asema Serikali haitawavumilia.
- Kuanza kuwatembelea Desemba mwaka huu.
- Hatua kali kuchukuliwa kwa watakaobainika.
Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk Dorothy Gwajima amewatumia salamu wamiliki wa vituo vya kulelea watoto mchana ambao hawajasajili vituo hivyo kuwa Serikali itawachukulia hatua kali za kisheria.
Dk Gwajima amesema kuwa Serikali haitovumilia kuona watu wanaanzisha na kuendesha vituo vya kulelea watoto mchana (Day care centers) bila kusajiliwa kwani kuna miongozo na namna za uendeshaji wa vituo hivyo.
“Niwape tu salamu ndugu zangu wale mlioanzisha vituo vya kulelea watoto mchana, nikija kukagua vituo hivyo tusikimbiane. Nitakuja kuanzia Desemba mwaka huu semeni ukweli tu hujasajiliwa ili upate elimu uelewe usajili kituo chako” amesema waziri huyo.
Dk Gwajima alikuwa akizungumza leo Oktoba 29, 2021 katika Tamasha la Karibu Dodoma linalofanyika katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma kwa siku sita.
Ni kosa la jinai kuendesha kituo au shule ya kulea watoto bila usajili. Kanuni ya 4(1) ya Kanuni za Vituo vya Kulea Watoto Wadogo Mchana na Watoto Wachanga za Mwaka 2012, zinasema kuwa mtu hataendesha kituo cha kulea watoto wadogo isipokuwa kama anamiliki cheti halali cha usajili.
Baadhi ya sifa zinazohitajika ili kupata usajili wa kuendesha kituo cha kulea watoto ni pamoja na eneo ambapo kituo kitajengwa litatakiwa kukaguliwa na ofisa afya wa eneo husika na kutoa ripoti ya kuridhisha kuwa panafaa kwa ajili ya kulelea watoto. .
Kama eneo/jengo ambapo utaendeshea kituo ni la kupanga, basi hakikisha una mkataba wa pango ambao hauko chini ya miaka mitatu. Utatakiwa kuthibitisha uwezo wa kifedha kuwa unaweza kuendesha kituo.
Pia Hakikisha eneo lina vifaa vya kutosha kwa ajili ya michezo ya watoto, muombaji/waombaji wawe na akili timamu na kuthibitisha kuwa baada ya kupewa cheti cha kuendesha kituo hautatoa, kuuza, kukodisha kituo au cheti chako kwa mtu mwingine yeyote.
Picha za Matukio mbali mbali zikimwonesha Waziri wa Afya, Dk Dorothy Gwajima alipotembelea mabanda mbalimbali katika viwanja vya Chinangali, katika tamasha la ‘KARIBU DODOMA FESTIVAL, ambapo taasisi na hospitali za Taifa zimeshiriki na kutoa huduma za kibingwa na ushauri nasaha. Picha| Wizara ya Afya.
Aidha, Dk Gwajima amewataka wazazi na walezi nchini kuzingatia suala la malezi kwa watoto kwani ni jambo la msingi na linasaidia kuondokana na matatizo mengi ikiwemo watoto wanaoishi na kufanya kazi mtaani.
Amesema kuwa kuna wimbi la watoto wengi wanaokimbilia mitaani wanaotoka katika familia ikiwemo kukosa malezi, matatizo ya kifamilia na hata kunyang’anywa haki zao katika jamii kutokana na vifo vya wazazi au walezi wao.
Ameongeza kuwa nia ya Serikali ni kuhakikisha watoto wanapata haki zao za msingi na huduma muhimu zikiwemo elimu na afya huvyo wazazi na walezi wana wajibu wa kuhakikisha wanawapa malezi na matunzo stahiki watoto wao.
“Hii ni Wizara yangu nitahakikisha miongozo iliyopo hasa kuhusu watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani inatekelezwa kwa kupatikana mbinu sahihi ya kuwakusanya watoto na kuwaunganisha na familia zao na wale ambao hawana familia wanapata familia za kuwalea kwa njia ya kuasili,” amesem Dk Gwajima
Aidha Waziri Dkt. Gwajima amewataka watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani kutowakimbia watu wanaotaka kuwasaidia na kuwaunganisha na familia zao au kuwatafutia familia za kuwalea kwani ni njia ya kuwasaidia kuondokana na madhira ya kuishi na kufanya mitaani.
Aidha, amezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa kushirikiana na wadau mbalimbali katika maeneo yao kuwatambua watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani na kuwapatia msaada ili kuondokana na tatizo hilo katika mameno yao na kufanya watoto waishi katika mazingira salama na rafiki.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe. Jabir Shekimweli amesema kuwa Wilaya ya Dodoma itashirikiana na Wizara kuhakikisha inaweka utaratibu sahihi wa kuwatambua na kuwaunganisha familia zao, watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani ikiwemo kuweka utaratibu mzuri wa kuwa na eneo litakalotumika kuwakusanya.
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeshiriki tamasha la Karibu Dodoma huku ikishirikisha Taasisi zake zote mbazo zilimetoa huduma kwa wananchi wa Dodoma na mikoa ya karibu zikiwemo huduma za uchunguzi wa macho, moyo na matibabu ya kibingwa.
Latest