Ajali ya treni ya abiria yaua wanne Tabora
Treni ya abiria iliyokuwa ikisafiri kutoka Kigoma kuelekea jijini Dar es Salaam imepata ajali majira ya saa tano asubuhi, katika eneo la Malolo mkoani Tabora na kusababisha vifo vya watu wanne na majeruhi 132. Picha| Yusuph Jackson.
- Treni ya abiria iliyokuwa ikisafiri kutoka Kigoma kuelekea jijini Dar es Salaam.
- Imesababisha vifo vya watu wanne na majeruhi 132.
- Chanzo cha ajali bado hakijajulikana.
Dar es Salaam. Treni ya abiria iliyokuwa ikisafiri kutoka Kigoma kuelekea jijini Dar es Salaam imepata ajali majira ya saa tano asubuhi, katika eneo la Malolo mkoani Tabora na kusababisha vifo vya watu wanne na majeruhi 132.
Kati ya waliofariki, watoto chini ya miaka mitano ni wawili na watu wazima wawili.
Shirika la Reli Tanzania (TRC) katika taarifa yake iliyotolewa leo Juni 22, imesema treni hiyo yenye namba Y14 iliyobeba abiria 930 ilipata ajali leo eneo la Malolo mkoani Tabora, kilometa 10 kutoka kituo cha treni cha Tabora.
“Behewa tano za abiria daraja la tatu, behewa moja la vifurushi, behewa moja la huduma ya chakula na vinywaji na behewa la breki, zilianguka na kusababisha ajali,” imeeleza taarifa hiyo.
Majeruhi wa ajali hiyo tayari wamefikishwa katika Hospitali ya Mkoa ya Kitete iliyopo mkoani Tabora, ambapo hali zao zinaendelea vizuri.
“Majeruhi 132 tayari wamefikishwa hospitali ya mkoa Kitete-Tabora na wanaendelea vizuri,” imeeleza TRC.
TRC imesema chanzo cha ajali hiyo bado hakijafahamika, wameanza kufanya uchunguzi ili hatua zaidi ziweze kuchukuliwa.
Aidha TRC imesema walionusurika na ajali hiyo wameanza kusafirishwa kutoka Tabora ili kuendelea na safari ya kurudi Dar es salaam.
Ajali hiyo treni ni ya tatu kwa mwaka huu ambapo Mei 9, treni ya abiria namba I13 ilipata ajali katika stesheni ya Mpiji mkoani Pwani na hakukua na majeruhi wala kifo.
Ajali nyingine iliyohusisha treni ya abiria ya TRC ilitokea Januari jijini ikuhusisha daladala kuligonga treni linalotoa huduma katika ya Kamata na Pungu katika eneo la Banana ambapo watu wawili walifariki dunia na majeruhi sita ambao walitibiwa na kuruhusiwa kuendelea na shughuli zao.