Nukta Africa, Internews wazindua mafunzo ya uandishi wa habari za takwimu Tanzania

October 10, 2022 9:10 am · Davis Matambo
Share
Tweet
Copy Link
  • Mafunzo hayo ya mtandaoni yanafanyika leo Oktoba 10 hadi 12, 2022.
  • Lengo ni kuwamengea uwezo wa kuandika kwa ufasaha habari za takwimu. 
  • Wanawake watakiwa kujitokeza zaidi katika mafunzo hayo. 

Dar es Salaam. Kampuni ya habari na teknolojia ya Nukta Africa kwa ushirikiano na Shirika la Internews wamezindua mafunzo maalum kwa waandishi wa habari Tanzania ili kuwawezesha kuandika kwa ufahasa habari za takwimu na zenye mchango mkubwa katika maendeleo.

Mafunzo hayo ya mtandaoni yatafanyika kwa siku tatu kuanzia leo Oktoba 10 hadi 12, 2022. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Nukta Africa, Nuzulack Dausen akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo ya wanahabari wa vyombo mbalimbali Tanzania amesema mafunzo hayo ni adimu na ghali na kuwataka waandishi waliopata fursa kuyatumia vizuri ili wafaidike nayo. 

“Ni moja ya mafunzo adimu, ghali na hayatolewi kwa muda mrefu…myathamini (washiriki wa mafunzo) na muwe makini muda wa kujifunza,” amesema Dausen.

Dausen amesema licha ya mafunzo hayo kuwa na umuhimu, bado washiriki wanawake ni wachache kwa sababu muitikio wao ni mdogo kila fursa zinapotangazwa. 

Amesema habari za takwimu zina mchango mkubwa kwenye jamii, endapo waandishi watazipa kipaumbele. 

Mafunzo hayo ni sehemu ya mradi wa miezi tisa wa Boresha Habari unaofadhiliwa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Uswisi na Shirika la Misaada la Watu wa Marekani (USAID) ambao unaolenga kuongeza uelewa kuhusu uthibitishaji habari na jinsi ya kuandika habari za takwimu kwa wanahabari.

Pia mradi huo utazifaidisha asasi za kiraia (Azaki) kuzijiwengea uwezo wa kuthibitisha habari katika shughuli zao kila siku ili kuepuka habari za uongo na kuunda madawati ya wathibitishaji habari kwenye vyombo vya habari vya sita vya kitaifa. 


Soma zaidi


Mtaalam wa Vyombo vya Habari wa Internews, Alakok Mayombo  amewapongeza wakufunzi wa Nukta Africa kwa mwendelezo wa kutoa mafunzo hayo kila mwaka na kuwasisitiza washiriki wa mafunzo hayo ya uandishi wa habari za takwimu kushiriki kikamilifu kipindi chote cha mafunzo.

“Wote tunafahamu dunia inavyokua, suala la uandishi wa hadari za takwimu halikwepeki. Ukweli na usahihi unakua wa uhakika na kufanya mambo mengi yaeleweke zaidi kwa kutumia data,” amesema Mayombo. 

Mayombo amesema tangu waanze kutoa mafunzo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Nukta Africa, yamesaidia kuongeza mchango wa tasnia ya habari katika maendeleo ya Taifa. 

“Uandishi wa habari za data unakuza umahiri na ueledi, tumekuwa na mafunzo haya kwa zaidi ya miaka mitano iliyopita, wengine wamepata tuzo ya Excellence Journalism Awards (Tuzo za Umahiri wa Uandishi wa Habari (EJAT))” amesema mwandishi huyo mkongwe.

Nukta Africa katika utekelezaji wa mradi huo itakuwa na majukumu mbalimbali ikiwemo kufundisha wanahabari  na asasi za kiraia kuhusu uandishi wa habari za takwimu na  uthibitishaji habari.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW