Waziri Mkuu wa Uingereza ajiuzulu baada ya kukaa ofisini kwa siku 45
- Amesema asingeweza kutimiza ahadi alizotoa alipokuwa akiwania nafasi ya kuwa kiongozi mkuu wa chama cha Conservative ili kumuwezesha kuwa waziri mkuu.
Dar es Salaam. Liz Truss, Waziri wa Uingereza amejiuzulu muda mfupi uliopita na kuweka historia ya waziri mkuu aliyekaa madarakani muda mfupi nchini humo.
Kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Waziri Mkuu wa pili aliyehudumu kwa muda mfupi zaidi alikuwa George Canning, alihudumu kwa siku 119 baada ya kufariki dunia.
Trus katika hotuba yake ya kujiuzulu leo Oktoba 20, 2022 mbele ya ofisi yake amesema asingeweza kutimiza ahadi alizotoa alipokuwa akiwania nafasi ya kuwa kiongozi mkuu wa chama cha Conservative ili kumuwezesha kuwa waziri mkuu.
“Tuliweka maono ya kodi ya chini na wa ukuaji wa juu wa uchumi ambao utachukua fursa ya uhuru wa Brexit.”
“Lakini ninatambua, kutokana na hali hiyo, siwezi kutoa mamlaka ambayo nilichaguliwa na Chama cha Conservative. Kwa hiyo nimezungumza na Mtukufu Mfalme kutangaza kwamba ninajiuzulu kama kiongozi wa Chama cha Conservative,” amesema.
Duru za kimataifa zinaeleza kuwa kujiuzulu kwake kumetokana kufeli kwa mpango wake wa kiuchumi uliosababisha mtikisiko wa masoko ya kifedha na kukigawa chama chake.
Kujiuzulu kwake kumetanguliwa na mfululizo wa matukio ya fujo ndani ya chama chake ambapo baadhi ya wanachama wamekuwa wakimshinikiza ajiuzulu, licha ya yeye kutotaka kufanya hivyo.
Jana jioni Oktoba 19, 2022 Waziri wa Mambo ya Ndani Suella Braverman, alijiuzulu akiwa ni waziri wa pili kuondoka katika baraza la mawaziri la Waziri Mkuu Liz Truss.
Mapama leo asubuhi, waziri mwingine aliwasilisha barua ya kutokuwa na imani na Trus.
Waziri Mkuu mpya anatarajiwa kuteuliwa wiki ijayo. Hata hivyo, kiongozi wa upinzani Keir Starmer ametaka uchaguzi mkuu ufanywe.
Truss alichukua wadhifa huo baada ya Boris Johnson ambaye pia alilazimika kujiuzulu kutokana na kashfa mbalimbali ikiwemo kukiuka kanuni za kujikinga na Uviko-19.