Zijue faida, hasara za kufanya malipo kwa njia ya mtandao
- Zitakusaidia kufanya maamuzi ya namna ya kutumia pesa zako.
- Inakupa uzoefu wa kutumia mifumo ya teknolojia inayovumbiliwa.
Dar es Salaam. Malipo ya bidhaa na huduma kwa njia ya mtandao yanashika kasi duniani, jambo linatoa fursa kwa kampuni za teknolojia zikiwemo za simu kuwawezesha wateja wao kufanya malipo popote walipo bila hata kuhitaji kubeba pesa taslimu.
Huduma hizo ni kama “Lipa kwa M-pesa”, Mastercard, Visa, Tigo pesa na nyingine nyingi ambazo pia zimekuwa kiungo muhimu cha biashara ya mtandaoni.
Huduma hizi zimechochea kasi ya shughuli za kiuchumi na kijamii na kuondoa changamoto mbalimbali za malipo hasa ya benki ambazo hazijaenea kila mahali nchini.
Hata hivyo, wakati ukitumia ni muhimu kufahamu faida na hasara kama siyo changamoto za kutumia mifumo ya mtandaoni kufanya malipo. Kwa upande faida:
Inakuhakikishia usalama wa pesa zako
Moja ya umuhimu uliopo katika kutumia huduma hizo ni pamoja na usalama wa kutembea na pesa nyingi popote unapokuwa. Huenda pindi unapotembea na pesa nyingi mfukoni ukakosa amani kwa kuhofia kuporwa au kuibiwa.
Ila kwa uwepo wa huduma hizo usalama wa pesa unaongezeka kwa kiasi kikubwa kwani pesa zimehifadhiwa kwenye mfumo usiokuwa rahisi kuingiliwa na mtu mwingine tofauti isipokuwa kwa namba ya siri unayoifahamu mwenyewe.
Ni njia ya haraka kufanya malipo
Ni wazi kwamba malipo kwa njia ya mtandao ni ya haraka zaidi kwani kuliko kusubiri kuja kuhudumiwa na mtu kwa kupokea pesa taslimu.
Inaokoa muda kwa sababu malipo yanafanyika mtandaoni na kuharakisha shughuli zako hasa kama ni mfanyabiashara.
Malipo ya mtandaoni ni njia rahisi ya kupata bidhaa au huduma kwa haraka mtandaoni. Picha|Republic
Inaongeza ujuzi wa kutumia huduma mbalimbali za malipo
Unapokwenda kutembea nchi nyingine ambapo hutumia teknolojia ya malipo kwa njia ya mtandao inakupa urahisi kustahimili mazingira hayo kwani kinakuwa kitu ulichozoea na siyo kigeni kufanya matumizi, kuliko unapoanza kukitumia kwa mara ya kwanza huenda ikakuletea shida katika mazingira ya ugenini.
Hata wakati ukiendelea kufurahia faida za huduma za malipo ya bidhaa mtandaoni. Ni muhimu pia kufahamu changamoto zinazotokea katika mifumo hiyo ili ujiweke katika nafasi nzuri ya kukabiliana nazo.
Inaongeza gharama za ziada
Kwa kutumia malipo ya mtandaoni, uwezekano wa kuingia gharama mara mbili ni mkubwa kuliko kutumia nyia ya malipo ya kawaida kwa pesa (Cash) kwani unapofanya muamala kwa huduma au mtandao husika kuna makato unayoweza kuingia kuliko ukitumia njia za kawaida.
Mfano mtu anapofanya manunuzi ya bidhaa inayouzwa Sh10,000 ni wazi kwamba kwa kutumia pesa taslimu atalipa 10,000 pekee, ila akitumia malipo ya mtandao atalipa pesa ya bidhaa pamoja na gharama ya makato kulingana na huduma anayotumia.
Inaweza kuwa chanzo cha kutumia pesa bila mpangilio
Kwa mazoea ya kutembea na kadi ya malipo, unaweza kutumia pesa ambazo hukuziwekea bajeti pale tu unapovutiwa na kitu fulani.
Hii ni tofauti na matumizi ya pesa ya kawaida ambapo unaweza kukosa pesa ya kufanya manunuzi kwa wakati huo mpaka uende kuitoa kwenye akaunti au kufanya mchakato mrefu ambapo huenda mtu akakata tamaa na kuokoa pesa yake.
Kwa kutambua faida na hasara za teknolojia hiyo ni rahisi mtu kufanya uamuzi wa kutumia mtandao kufanya malipo au njia ya kawaida kuhakikisha pesa zinatumika ipasavyo kulingana na mipango ya mtu.
Kuna teknolojia nyingi zinazoweza kukusaidia kufanya maamuzi katika nyanja mbalimbali za maisha, usikose kusoma Nukta jumatatu ijayo.