Watanzania waishio nje ‘watasubiri sana’ kushiriki uchaguzi wa ndani
- Serikali imesema bado inaandaa sera na ikikamilika italijulisha Bunge na wananchi wote.
- Imesema inatathmini idadi ya Watanzania waliopo nje na shughuli wanazofanya.
- Huenda Watanzania hao wasipate fursa ya kushiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka huu.
Dar es Salaam. Watanzania wanaoishi nchi za nje wataendelea kusubiri kwa muda usiojulikana kupata fursa ya kushiriki chaguzi za ndani wakiwa nje baada ya Serikali kusema kuwa bado inaandaa sera na kutathmini ili kuona kama utaratibu huo unafaa.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa leo (Mei 23, 2019) wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti maalumu (CCM), Asha Juma aliyetaka kujua ni lini Serikali itakamilisha utaratibu wa kuwawezesha Watanzania wanaoishi nchi za nje kuweza kupata nafasi yao ya kidemokrasia ya kupiga kura.
“Jambo hili ni la kisera na Serikali imeendelea kuona kama utaratibu huo unaweza kufaa kwa sababu lazima tupate kujua nani wako nje ya nchi, idadi yao, wanafanya shughuli gani, na je kama bado ni Watanzania au waliomba urai wa kule nchi za nje,” amesema Majaliwa.
Soma zaidi:
- Majaliwa: Nawaonya watu wote wanaotumia vibaya mitandao ya kijamii waache
- Majaliwa aagiza elimu itolewe upangaji madaraja ya korosho.
Majaliwa amesema pindi sera hiyo itakapokamilika pale itakapoonekana inafaa, Serikali itawajulisha Watanzania na Bunge.
Hata hivyo, Waziri Mkuu hajawaweka wazi ni lini sera hiyo itakamilika, jambo ambalo linawaweka katika wakati mgumu Watanzania hao waishio nje kama wanaweza kushiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika mwaka huu na Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika mwaka 2020.