Watakaohujumu SGR, bandari, meli Kigoma kumulikwa
- Rais Samia awataka wananchi kuitunza miundombinu hiyo kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu amezindua ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora–Kigoma pamoja na meli nne za mizigo katika Bandari ya Karema, mkoani Kigoma hatua inayotajwa kuchochea ukuaji wa uchumi.
Baada ya kukagua na kuzindua miundombinu hiyo Rais Samia ameonya hujuma zinazofanyika dhidi ya miundomboinu hiyo akisistiza kuwa vitendo hivyo ni hasara kwa Taifa na vizazi vijavyo.
“Hujuma yoyote dhidi ya miundombinu hii si hasara kwa Serikali pekee, bali ni kwa kila Mtanzania na kwa kizazi kijacho. Bila usalama hakuna maendeleo,” amesema Rais Samia leo Julai 20,2026.
Reli hiyo yenye urefu wa kilomita 506 itagharimu takribani Sh7.4 trilioni, ikitarajiwa kuunganisha mkoa wa Kigoma, Tabora, Dodoma, Morogoro na Dar es Salaam pamoja na mtandao wa reli unaoelekea Mwanza.

Hata hivyo, kiongozi huyo wa nchi hakuweka wazi ni lini reli hiyo inatarajiwa kukamilika licha ya kuwepo uhitaji mkubwa wa usafiri wa haraka kanda ya magharibi mwa Tanzania.
Kipande cha SGR cha Tabora–Kigoma kinakamilisha hatua ya kuzindua vipande vyote sita vya mradi wa reli hiyo nchini tangu ulipoanza kutekelezwa rasmi Mei, 2017.
Mpaka sasa, vipande viwili vya Dar es Salaam–Morogoro na Morogoro–Makutupora tayari vinatoa huduma, huku vingine vikiendelea na ujenzi
Ni uwekezaji wa mfano
Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amebainisha kuwa ujenzi wa meli nne za mizigo katika Ziwa Tanganyika ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha usafiri wa majini na kutumia fursa za kibiashara zilizopo katika nchi jirani ikiwemo Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Burundi na nchi nyingine zinazozunguka Ziwa Tanganyika.
Kila meli ina uwezo wa kubeba tani 2,000 za mizigo, huku mradi huo ukiongeza uwezo wa Bandari ya Kigoma kutoka kuhudumia tani 800,000 hadi tani milioni mbili kwa mwaka.