Wasichana walivyokimbiza matokeo kidato cha sita 2022
- Wafanya vizuri zaidi katika masomo ya sayansi na biashara.
- Wavulana wajitetea masomo ya sanaa na lugha.
Dar es salaam. Wakati leo watu wakisheherekea na kuhuzunika baada ya kutangazwa kwa matokeo ya mtihani wa kidato cha sita kwa mwaka 2022, wasichana wamefanya vizuri zaidi katika masomo ya sayansi.
Kwa mujibu wa matokeo hayo yaliyotangwa leo Julai 7, 2022 na Kaimu Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Athuman Amas, nafasi saba kati ya 10 katika orodha ya wanafunzi waliofanya vizuri kitaifa katika masomo ya sayansi zimechukuliwa na wasichana.
Katika orodha hiyo ya dhahabu kwa masomo ya sayansi, namba moja imeshikiliwa na Catherine Alphonce Mwakasege aliyesoma tahasusi ya PCB kutoka shule ya St. Mary’s Mazinde juu iliyopo mkoani Tanga akifuatiwa na Lucy E. Magashi kutoka shule hiyo hiyo ambayo imeingiza wasichana wote saba waliofanya vizuri.
Nafasi ya tatu imeenda kwa Mhewa Charles Kamando kutoka Shule ya Tabora Boys’ iliyopo mkoani Tabora huku Norah Eliaza Kidjout akishika nafasi ya tano.
Soma zaidi:
-
Matokeo kidato cha sita 2022 yatangazwa, ufaulu waongezeka kidogo
- Matokeo kidato cha sita 2022 haya hapa
Jennifer Martin Chuwa ameshika nafasi ya sita akifuatiwa na Paulina Aldephonce Mabamba na Rachel Joachim Moshy katika nafasi ya nane.
Nafasi ya tisa imeenda kwa Kulwa Mbizo Elias wa Tabora Boys’ huku Oscar Eliakimu Malabe wa shule hiyo akifunga orodha ya 10 bora ya wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo ya sayansi.
“Watahiniwa waliofanya vizuri zaidi kitaifa wamepatikana kwa kulinganisha jumla ya pointi kwenye masomo ya tahasusi (combination) pamoja na wastani wa alama za jumla walizopata,” amesema Amas.
Hata katika masomo ya biashara, wasichana wamewagaragaza wavulana. Necta imeeleza kuwa katika 10 bora ya masomo hayo, nafasi tisa zimechukuliwa na wasichana.
Wavulana watamba masomo ya sanaa na lugha
Hata hivyo, wakati wasichana wakitamba katika masomo ya sayansi na biashara, wavulana nao wameonesha umwamba katika masomo ya sanaa na lugha.
Katika orodha ya watahiniwa 10 waliofanya vizuri zaidi katika masomo ya sanaa na lugha wavulana ni sita na wasichana ni wanne.
Hamza Masudi Ngosse ambaye amesoma tahasusi ya HGK katika shule ya Sekondari Songea Boys’ iliyopo mkoani Ruvuma ndiye kinara katika orodha hiyo.
Latest
