Wanawake walioolewa, wenye watoto ruksa kushiriki ‘Miss Universe’

October 5, 2022 11:47 am · Davis Matambo
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni baada ya waendeshaji kubadili kanuni.
  • Hiyo itattoa fursa kwa wanawake kushiriki kwa wingi mashindano hayo.
  • Wataanza kushiriki katika mashindani ya mwaka 2023.

Dar es Salaam. Huenda mashindano ya ulimbwende yanayofanyika katika maeneo mbalimbali duniani yakachua sura mpya na kufungua fursa zaidi kwa wanawake kufaidika na tasnia hiyo baada ya kufanyika kwa mabadiliko kadhaa kwa washiriki.

Shirika la ‘Miss Universe’ lenye makao yake nchini Marekani, ambalo huendesha shindano mlimbwende wa dunia la Miss Universe, limeruhusu wanawake waliozaa watoto na walioolewa kushiriki mashindano hayo kuanzia mwakani.

Awali kwa mujibu wa kanuni za shirika hilo, washiriki wa taji hilo walikuwa wanawake ambao hawajaolewa wala kuzaa wenye umri kati ya miaka 18 hadi 28.

Pia mshindi wa jumla alitakiwa kuwa bachela katika kipindi chote cha kushikiria taji lake.

Hata hivyo, kuanzia mwaka ujao, hali ya ndoa au uzazi haitakuwa miongoni mwa vigezo vya kumfanya mtu ashiriki mashindano hayo.

Mshindi wa Miss Universe mwaka 2020 Andrea Meza wa Mexico amesifu mabadiliko mapya ya kanuni na amekosoa miongozo ya sasa kuwa “ya kijinsia” na “isiyo halisi” katika juhudi za kuchagua mshindi ambaye anavutia hadhira kubwa zaidi.

“Watu wachache wanapinga mabadiliko haya kwa sababu siku zote walitaka kuona mrembo mmoja ambaye anapatikana kwa uhusiano,” Meza ameongeza kuwa “siku zote walitaka kuona mwanamke ambaye ni mkamilifu sana kwamba hawezi kufikiwa karibu.”

Huenda katika mashindano ya 72 yatakayofanyika nchini Colombia mwakani, mwanamke mwenye mtoto au aliyeolewa atachukua taji hilo baada ya vikwazo kuondolewa.

Wanawake kutoka nchi 80 hushiriki mashindano hayo kila mwaka. Tukio hilo la aina yake hutangazwa katika mipaka na nchi 160 duniani.

Shindano la kwanza la Miss Universe lilifanyika mwaka 1952 California nchini Marekani.

Hata hivyo, Armi Kuusela kutoka Finland ambaye alikuwa mshindi wa kwanza katika mashindano hayo alivuliwa taji hilo baada ya kukiuka masharti na kuamua kuolewa kabla ya muda wa kushikilia taji lake kuisha.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW