Uthubutu, teknolojia ya kisasa kuwabeba wawekezaji wazawa
- Serikali yasema hakuna mwananchi asiyeweza kuwekeza kikubwa ni kuwa na nia na uthubutu.
- Waziri Kairuki awataka Watanzania waache kukatishana tamaa katika kuibua miradi ya uwekezaji.
Dar es Salaam. Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya uwekezaji, Angellah Kairuki amewataka wananchi kuthubutu na kutumia teknolojia ya kisasa kuwekeza katika maeneo yenye tija nchini Tanzania ili kujikwamua kiuchumi na kujiletea maendeleo.
Ametoa hamasa hiyo kwa Watanzania kuzichangamkia fursa na kuwatoa shaka kuwa hakuna mwananchi asiyeweza kuwekeza kikubwa ni kuwa na nia na uthubutu.
“Ni ukweli kuwa, kila uwekezaji Mtanzania anaweza kuufanya muhimu kuwa na ujuzi, teknolojia pamoja na mtaji pasipo kutia shaka na kujiamini,”amesema Waziri Kairuki alipotembelea kiwanda cha kuchakata maziwa ya mtindi cha Mather Dairies kilichopo Kijiji cha Ikwiriri, Wilaya ya Rufiji katika Mkoa wa Pwani Januari 23, 2020.
Ikiwa uwezo wa kuwekeza ni mdogo kwa kuzingatia ukosefu wa ujuzi, amesema wananchi wanapaswa kutumia fursa za mafunzo ya ukuzaji ujuzi yanayotolewa katika vyuo mbalimbali na kutumia watu wenye uzoefu inapofaa kulingana na aina ya uwekezaji wanaotaka kuufanya.
“Kumekuwa na tabia ya kukatishana tamaa pindi mtu anapothubutu kuona fursa na kuichangamkia, ni rai yangu kwa wananchi kuona Watanzania tunawekeza kufanya mambo makubwa katika maeneo yote yenye fursa, na kuzitumia vyema mamlaka zilizopo kwa kupata msaada ya ushauri elekezi na miongozo ya namna bora ya kuwekeza,” amesema Kairuki katika taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Zinazohusiana:
- Sababu zilifanya Tanzania iporomoke viwango vya ufanyaji biashara duniani
- Sekta binafsi yazungumzia Kairuki kuteuliwa kusimamia uwekezaji
Akiwa katika kiwanda hicho kilichowekeza mtaji wa zaidi ya Sh300 milioni kina uwezo wa kuchakata zaidi ya lita 2,000 kwa siku ambazo hutengeneza maziwa ya mtindi aina ya “Yogurt Full”.
Kiwanda hicho kimeweza kusaidia zaidi ya vijana 12 ambao wamekuwa wakizalisha na kuuza maziwa maeneo mabalimbali nchini ikiwemo; Masasi, Kibiti, Rufiji, Mtwara na Dar es Salaam.
Latest