“Ubongo wa mwanamke umechangamka zaidi kuliko wa mwanaume”

August 21, 2018 6:40 pm · Zahara
Share
Tweet
Copy Link
  • Utafiti unaonyesha kuwa wanawake wana uwezo wa kufanya vitu vingi kwa wakati mmoja kuliko wanaume.
  • Sehemu za ubongo za mwanamke zimechangamka sana kuliko mwanaume.
  • Hii ndio sababu nyingine ya wanawake wengi kupata sonona, wasiwasi au matatizo ya kupenda au kutokupenda kula.

Umewahi kujiuliza kwanini wanawake wanaweza kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja, kitu ambacho wanaume wengi hawawezi? Haya yanaonekana zaidi hata katika maeneo ya kazi, utakuta mwanamke anamajukumu ya kazi bado anahakikisha anahudumia familia na kujihusisha na matukio mbalimbali kwa wakati mmoja.

Hata katika mazingira ya nyumbani ni rahisi kumuona mwanamke akiwa amembeba mtoto mgongoni wakati akipika na wakati huohuo anaweza kufanya jambo lingine.

Utafiti mpya uliotolewa hivi karibuni umebaini kuwa sehemu nyingi za ubongo wa mwanamke zimechangamka zaidi kuliko za mwanaume jambo linalomfanya ajishughulishe na mambo mengi kwa wakati  mmoja.

Ripoti ya utafiti uliofanywa na wanasayansi kutoka kliniki ya Amen (Amen Clinics) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha California iliyotolewa mwaka 2017 ilitumia sampuli 46,034 za ubongo kutoka kwa wagonjwa 26,683 kwenye  vituo tisa na kufanya uchambuzi wa jinsi ubongo wa mwanamke na mwanaume unavyofanya kazi. 

                                Sehemu ya ndani ya ubongo kwa mwanamke na mwanaume. Picha| Mtandao.

Baada ya uchambuzi wa kina wamebaini kuwa sehemu za ubongo wa mwanamke zimechangamka au zinafanya kazi  kuliko mwanaume hasa ubongo wa eneo la mbele la ubongo wa mwanamke ambao upo kwa ajili ya kutoa maamuzi, hisia na kusimamia matendo na tabia ya mtu. 

Hata hivyo,  katika suala la kuona na kupanga vitu mwanaume yupo vizuri kuliko mwanamke jambo linalomfanya achukue muda mrefu kupangilia mambo na kufanya maamuzi.

Walibaini kuwa kinachofanya ubongo wa wanawake kuchangamka zaidi ni mzunguko mkubwa wa damu katika ubongo kuliko wanaume jambo linalowasaidia kufanya mambo kwa haraka na kuonyesha matokeo chanya kwa muda mfupi. 

Pamoja na sifa hizo za ubongo wa wanawake, bado wana changamoto ya kupata msongo wa mawazo, wasiwasi, sonona na matatizo ya kukosa usingizi ikiwa yale wanayoyafanya hajaleta matokeo wanayoyataka. Hali hiyo hutokana na ufanyaji mambo kwa hisia na haraka. 

Kwa wanaume hujipa muda ili kujiridhisha na jambo wanalotaka kufanya ambapo hufanya mambo machache kwa muda mrefu.

                                Mwanamke anaweza kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja huku akiwa na furaha lakini uwezo huo humfanya awe dhaifu zaidi kukabiliana na msongo wa mawazo na sonona pale mambo yanapoenda tofauti. Picha | busywifebusylife.

Uwezo mdogo wa uchakataji taarifa kwa wanaume ndani ya muda mfupi umewafanya wakati mwingine kukosa umakini na kutunza muda kwa mambo wanayoyafanya (ADHD ‘Attention Deficit Hyperactivity Disorder). 

Tofauti za utendaji wa ubongo kati ya mwanamke na mwanaume zina faida hasa kwa madaktari wa magonjwa ya ubongo kufahamu njia sahihi za kutoa tiba inayoendana utendaji wa ubongo wa mgonjwa.   

Matokeo ya utafiti siyo mwisho wa kutafiti zaidi juu ya utendaji wa ubongo wa mwanamke na mwanaume, ikizingatiwa kuwa ubongo wa binadamu unabadilika kulingana na mazingira anayopitia katika maisha yake. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW