Treni la Dar, Moshi kurejea tena ndani ya siku 14
- Zilisitishwa kwa muda kutokana na uharibifu wa reli uliosababishwa na mafuriko.
- Kazi ya ukarabati wa kipande za reli kati ya stesheni ya Buiko na Hedaru inaendelea.
Dar es Salaam. Wakazi wa mikoa ya kaskazini mwa Tanzania ambao hutumia treni kutoka Dar es Salaam wataanza kuutumia tena usafiri huo baada ya Shirika la Reli Tanzania (TRC) kutangaza kurejesha huduma hizo ndani ya siku 14 zijazo.
TRC imesema safari za treni ya mizigo na abiria kati ya jiji la Dar es Salaam na mkoa wa Kilimanjaro zitarejea baada ya kusitishwa kwa usafiri huo kwa muda kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na kujaa kwa mto Pangani.
Mto huo ambao uko mkoani Tanga ulijaa kutokana na mvua zilizonyesha katika maeneo ya Mkoa wa Kilimanjaro na nchi jirani ya Kenya Mei 2020.
“Mafuriko hayo yamesababisha uharibifu wa miundombinu ya reli kati ya stesheni ya Buiko na Hedaru ambapo kipande cha reli chenye urefu wa kilomita 1.6 kilifunikwa na maji kwa zaidi ya siku 21,” imeeleza taarifa ya TRC iliyotolewa Alhamisi, Juni 4, 2020.
Soma zaidi: Safari zote za treni ya TRC kuishia Kamata Dar
Kutokana na hali hiyo TRC ilisitisha safari za treni katika mikoa mitatu ya Dar es Salaam, Tanga na Kilimanjaro tangu Mei 10 ili kupisha matengenezo ya eneo hilo kabla ya kuruhusu tena safari za treni.
“Shirika linaendelea na kazi ya kuinua tuta kati ya stesheni ya Buiko na Hedaru ambapo matengenezo yanatarajiwa kukamilika ndani ya siku 14 tangu kuanza kwa kazi hiyo Juni 1, 2020,” imeeleza taarifa hiyo iliyotolewa na Kitengo cha Habari na Uhusiano cha TRC.
Safari hizo za treni kutoka Dar es Salaam hadi Moshi zilirejea Desemba 6, 2019 baada ya kusitishwa kwa miaka 25.
Usafiri huo ulianza kuwa msaada kwa baadhi ya abiria na wafanyabiashara wa mikoa hiyo hususan kipindi cha msimu wa sikukuu za mwishoni mwaka jana kutokana na ongezeko la watu waliokuwa wakielekea katika ukanda huo wa kaskazini mwa nchi.
Latest