TPDC yaangazia visima vitatu vya mafuta bonde la Eyasi
- Shirika hilo limeanza kufanya utafiti wa mafuta katika bonde la Eyasi Wembere ukihusisha uchorongaji wa visima vitatu vya utafiti vyenye urefu wa mita 900.
- Visima hivyo vyenye urefu wa mita 900 vinapatikana katika Wilaya za Igunga, Meatu na Iramba.
Dar es Salaam. Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeanza kufanya utafiti wa mafuta katika bonde la Eyasi Wembere ukihusisha uchorongaji wa visima vitatu vya utafiti vyenye urefu wa mita 900, jambo linaloweza kutoa fursa kwa Tanzania kufaidika na uchumi wa mafuta hapo baadaye.
Miamba ya bonde hilo yenye mabonde madogo (sub basin) ya Wembere na Manonga Iinapatikana katika mikoa ya Tabora, Shinyanga, Singida na Simiyu.
Meneja Utafutaji wa Mafuta na Gesi kutoka TPDC, Venosa Ngowi amesema kisima namba moja kinachorongwa katika kijiji cha Kining’nila Wilaya ya Igunga huku kisima namba mbili na tatu vitachorongwa katika Wilaya za Meatu Mkoani Simiyu na Iramba Mkoani Singida.
Amesema kuwa utafiti huu unakuja kufuatia ukusanyaji taarifa za bonde hilo uliofanyika mwaka 2015 kwa kutumia ndege maalumu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Idara ya Habari-Maelezo, bonde la Eyasi Wembere lina miamba tabaka mizuri ambayo inaweza kutumika kwa ajili ya utafiti wa mafuta na gesi hivyo na uchorogaji huu wa visima vifupi vya utafiti ni awamu ya pili kufuatia utafiti wa 2015/2016.
Akizunguzmia mita zilizochorongwa katika kisima namba moja, tayari zimechorongwa mita 116 kati ya 300 zinazopaswa kuchorongwa.
Utafiti huo unakuja ikiwa imepita miaka miwili, tangu Rais John Magufuli na Rais wa Uganda, Yoweri Museveni walipotia saini makubaliano ya utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga.
Wachimbaji (drillers) kutoka Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ambao ndio wamepewa kandarasi ya kuchimba visima vya utafiti katika Bonde la Wembere wakiendelea na kazi. Picha|Maelezo.
Meneja Mradi wa Utafutaji Mafuta katika bonde la Eyasi Wembere, Sindi Mduhu amesema baada ya ukusanyaji takwimu za eneo hilo, kilichofanyika ilikuwa ni kuzichakata na kuzitafsiri ili kuweza kuona ni wapi palipo na miamba tabaka yenye kina kirefu ambacho kinaweza kutunza mafuta.
“Kijiji cha Kining’inila ni mojawapo ya eneo ambalo lilihalalishwa kama moja ya eneo ambalo uchorongaji wa visima unaweza kufanyika,” amesema Mduhu katika taarifa hiyo.
Tayari baadhi ya wanachi wa Kijiji hicho wameanza kuonja neema ya utafiti huo ambapo kuna baadhi yao wamepatiwa kazi mbalimbali zisizohitaji elimu kubwa kama vile upishi, ulinzi pamoja na vibarua.
Zinazohusiana:
- Sababu nne za kutofautiana kwa matumizi ya umeme majumbani
- Tanzania, Uganda sasa kukamilisha mikataba ya bomba la mafuta mapema 2019
Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dk James Mataragio aliyefika ene la utafiti, amesema utafiti huo unafanyika kwa matumaini kuwa Tanzania inaweza kugundua mafuta.
“Tunafanya Utafiti kwa kutegemea kwamba kwa kipindi kisichozidi miaka mitano huenda tukagundua mafuta na hivi leo nawadhibitishia Watanzania kwamba kazi hiyo inaendelea,” amesema Dk Mataragio.
Katika ushirikishaji makampuni ya ndani katika utafiti huo, Dk Mataragio amesema kazi yote inafanywa na TPDC kwa kushihirikiana na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ambalo ni shirika la Serikali na ndiye Mkandarasi Mkuu katika mradi huo.
Latest
