TMA yatoa neno dhoruba iliyotokea Arusha, Manyara juzi
- TMA imesema chanzo ni mkusanyiko wa mawingu yenye radi yaliyotengeneza mkondo wa mawingu.
- imesema kwa sasa hali ya hewa ipo kawaida na matukio kama hayo hujitokeza pale mawingu yenye radi yanapojikusanya na kutengeneza mkondo.
- Imeshauri watu kuzingatia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa kila siku.
Dar es salaam. Siku moja baada ya kutokea kwa dhoruba ya upepo katika baadhi ya maeneo yamikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imewatoa hofu wakazi wa mikoa hiyo na kuwataka waendelee na shughuli zao kwa sababu hali ya hewa iko vizuri.
Taarifa iliyotolewa na Mamlaka hiyo leo (Oktoba 2, 2019) imesema chanzo cha dhoruba iliyotokea jana katika mikoa hiyo ni mkusanyiko wa mawingu ya radi katika eneo dogo na hivyo kupelekea kutengenezwa kwa mkondo wa mawingu ambao ulianzia nchini Kenya na kuelekea kwenye maeneo yaliyofikiwa nao.
“Dhoruba hiyo ya upepo ilidumu kwa kipindi kisichopungua dakika 30 katika eneo husika. Hali hiyo ilifuatiwa na vipindi vya mvua na ngurumo kutokana na mawingu hayo,” imesomeka taarifa hiyo.
TAARIFA KWA UMMA. pic.twitter.com/EaDyBiyAmQ
— Tanzania Meteorological Authority (@tma_services) October 2, 2019
Pamoja na hayo, TMA imesema kwa sasa hali ya hewa ipo kawaida na matukio kama hayo hujitokeza pale mawingu yenye radi yanapojikusanya na kutengeneza mkondo.
TMA imeshauri wananchi waendelee kufuatilia taarifa za kila siku za hali ya hewa ambazo zinatolewa na mamlaka hiyo ili kuwa na ufahamu wa mambo yanayoendelea.