Tanzania yaruhusu ‘Ethanol’ kuuzwa nje ya nchi

October 1, 2020 12:20 pm · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni kemikali inayotumika kutengenezea vinywaji baridi.
  • Uzalishaji wake waongezeka na kukidhi mahitaji ya soko la ndani. 
  • Wazalishaji wa kemikali hiyo watakiwa kufuata sheria kuisafirisha nje ya nchi.

Dar es Salaam. Wazalishaji na wafanyabiashara wa kemikali aina ya Ethanol wana kila sababu ya kutabasamu kutokana na Serikali kufungua milango ya kuuza katika soko la kimataifa.

Kemikali hiyo hutokana na masalia ya baadhi ya mimea ikiwemo mahindi na ngano hutumika zaidi katika mchakato wa utengenezaji wa vinywaji baridi ukiwemo mvinyo.

Pia hutumika kuongeza ufanisi wa vyombo vya moto yakiwemo magari.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Profesa Riziki Shemdoe amesema kuwa wameruhusu uuzaji wa kemikali hiyo nje ya nchi kutokana na kuongezeka kwa uzalishaji ambao unakidhi mahitaji ya ndani.

Amesema licha ya kukidhi mahitaji ya ndani, bado kuna ziada ya Ethanol ambayo inaweza kuuzwa nje ya nchi. 

“Aidha, Mheshimiwa Waziri (wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa) amewataka wazalishaji na wasafirishaji wa Ethanol nje ya nchi kuendelea kufuata taratibu zote za kisheria kwa ajili ya kuuza bidhaa hiyo nje ya nchi,” amesema Prof Shemdoe katika taarifa yake iliyotolewa leo (Oktoba 1, 2020).

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ethanol ikitumiwa vizuri inaweza kuwa njia endelevu ya kupunguza uharibifu wa mazingira unaosababishwa na matumizi ya nishati ya mkaa.

UN inaeleza kuwa majiko ya kupikia yanayotumia nishati ya Ethanol ni njia rahisi ya kuhimiza jamii kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW