Tanzania kuunganisha mifumo ya uwekezaji kielektroniki
- Imeanza kufanya maboresho ya huduma za uwekezaji kwa kuunganisha mifumo ya kielektroniki kwa taasisi na idara 11 za Serikali.
- Itasaidia kurahisisha utoaji wa vibali na leseni za uwekezaji nchini.
Dar es Salaam. Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kimeanza kufanya maboresho ya huduma za uwekezaji kwa kuunganisha mifumo ya kielektroniki kwa taasisi na idara 11 za Serikali zinazotoa huduma kwenye kituo cha pamoja cha uwekezaji.
Maboresho hayo yatasaidia kurahisisha utoaji wa vibali na leseni za uwekezaji kwa kuunganisha mifumo hiyo ili kuwa na dirisha moja la uwekezaji nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa TIC Dk Maduhu Kazi amesema maboresho hayo yatasaidia kuongeza ufanisi katika kutoa huduma kwa wawekezaji na kuimarisha utendaji kazi wa kituo hicho.
“Kama mnavyofahamu, Mheshimiwa Rais (Samia Suluhu Hassan) alitoa maelekezo ya namna ya kuboresha huduma za uwekezaji, kikao hiki ni muendelezo wa utekelezaji wa majukumu hayo, tulishaanza kuyafanyia kazi, na sasa tunaendelea, lengo ni kutoa huduma bora zaidi za uwekezaji” amesema Dk Kazi.
Dkt Maduhu amefanya kikao cha pamoja na wakuu wa taasisi na idara za Serikali 11 zinazotoa huduma kwenye kituo cha huduma kwa wawekezaji cha pamoja (One Stop Facilitaion Centre) na kubainisha kuwa mchakato wa maboresho hayo unaendelea kufanyiwa kazi.
Zinazohusiana:
- Sababu zilifanya Tanzania iporomoke viwango vya ufanyaji biashara duniani
- Sekta binafsi yazungumzia Kairuki kuteuliwa kusimamia uwekezaji
- Uwekezaji miradi mipya washuka Tanzania
Dk Kazi amepokea taarifa ya hatua ambazo zimechukuliwa kwa kila taasisi na idara husika zikiwepo kila taasisi kufungua mfumo wa kielektroniki kwa ajili ya utoaji vibali na leseni mbalimbali.
Maboresho haya yanaelezwa kuwa yatawawezesha wawekezaji wanaowekeza nchini kupata huduma kwa muda mfupi na kwa kutumia gharama ndogo.
Baadhi ya Taasisi zilizoshiriki katika kikao hicho ni pamoja na Uhamiaji, Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA), Mamlaka ya Chakula na Dawa (TMDA), Mamlaka ya Mapato Tanzani (TRA), Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi).
Latest