Tanzania itavunja rekodi mashindano ya olimpiki 2024?

August 12, 2021 7:42 am · Herimina
Share
Tweet
Copy Link
  • Mara ya mwisho kuchukua medani ilikuwa mwaka 1980.
  • Mwaka huu, Tanzania imetoka kapa katika mashindano hayo.

Dar es Salaam. Limebaki kuwa jambo la kihistoria kwa Tanzania kutwaa medali katika mashindano ya Olimpiki tangu ilipovunja rekodi ya dunia mwaka 1980.

Licha ya kuwa Watanzania wamekuwa wakishiriki mashindano hayo kila mwaka hawajaweza kuvunja rekodi ya mwaka 1980 huku wenzao wa Kenya na mataifa mengine wakiendelea kutamba kwa medali mbalimbali.

Mashindano hayo ambayo huwakutanisha wachezaji kutoka nchi mbalimbali duniani hujumuisha michezo kama sarakasi, kuogelea, mbio na kuruka vihunzi.

Katika mashindano ya Olimpiki ya mwaka 2021 yaliyofanyika Tokyo nchini Japan, Tanzania iliwakilishwa na wakiambiaji watatu: Gabriel Geay na Alphonce Simbu ambao walishiriki katika mashindano ya mbio ndefu kwa wanaume, huku Alphonce akishika nafasi ya saba.

Failuna Mtanga alishiriki mashindano ya mbio ndefu kwa upande wa wanawake ambapo alishika nafasi ya 24.

Historia ya Tanzania katika mashindano ya Olimpiki

Kwa mara ya kwanza, Tanzania ilipeleka washiriki katika mashindano ya Olimpiki mwaka 1964. Waliwakilishwa na wakimbia mbio Pascal Mfyomi, Hassan Chabanga, Omari Abdallah na Daniel Thomas, ambao hawakufanikiwa kufuzu katika mashidano ya mwaka huo.

Mwaka 1980, historia iliandikwa nchini baada ya washiriki wa mbio ndefu, Filbert Bayi na Suleiman Nyambui kuipeperusha bendera ya Tanzania katika mashindano ya Olimpiki ya mwaka huo yaliyofanyika Moscow nchini Urusi.

Wawili hao walitwaa medali mbili za shaba, Bayi akiwa ni mshindi wa kwanza wa mbio za mita 3,000 na Nyambui akiwa mshindi wa pili wa mbio za mita 5,000, akiwa sekunde moja nyuma ya mshindi wa kwanza, Miruts Yiftur kutoka Ethiopia.

Bendera ya Tanzania ikiwa imebebwa katika mashindano ya Olimpiki 2021 mjini Tokyo, Japan. Picha| Insidethegames. 

Baada ya medali hizo, Tanzania imekuwa ikipeleka washiriki Katika mashindano hayo na kurudi kapa, ikiwemo mashindano ya Olimpiki ya mwaka 2016 yaliyofanyika Rio de Janeiro nchini Brazil.

Mwaka huo, Tanzania ilipeleka washiriki saba  akiwemo Alphonce Simbu aliyeshika nafasi ya tano katika mashindano ya mbio ndefu.

Kamati ya olimpiki Tanzania (TOC) kupitia ukurasa wake wa mtandao wa Twitter, iliwahi kuandika ujumbe uliosomeka “Jambo la msingi sana kwenye mashindano ya Olimpiki siyo kushinda bali kushiriki. Kama ilivyo kwenye maisha, msingi siyo kushinda bali kupambana. Hii ni imani ya mashindano ya Olimpiki.”

Mashindano ya Olimpiki ya mwaka yalianza rasmi Julai 23 na kumalizika Agosti 8, na yalifanyika bila mashabiki kutokana na mwenendo wa ugonjwa wa virusi vya Corona (Uviko-19) duniani. 

Katika mashindano hayo, Marekani imeongoza kwa kuchukua medali nyingi, ambapo imechukua jumla ya medali 113, ikifuatiwa na China yenye medali 88.

Kwa bara la Afrika ni nchi 13 tu  ndizo zilizofanikiwa kutoka na medali katika mashindano hayo, ikiwemo Kenya ambayo imechukua jumla ya medali 10, ikifuatiwa na Egypt yenye medali sita. 

Mashindano hayo yanatarajiwa kufanyika tena mwaka 2024 nchini Ufaransa. Tanzania itavunja rekodi ya mwaka 1980?

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW