Shule za msingi, sekondari zanufaika na Sh83.2 bilioni kutoka Serikalini

- Kati ya fedha hizo, Sh38.6 bilioni zimepelekwa katika shule za msingi na Sh44.6 bilioni zimeenda katika shule za sekondari ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa utoaji elimu bila malipo.
- Zimetolewa kati ya Julai na Oktoba, mwaka huu ili kuimarisha usimamizi na uendeshaji wa shule hizo ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi.
Dar es salaam. Serikali imetoa Sh83.2 bilioni ili kuimarisha usimamizi na uendeshaji wa shule za msingi na sekondari nchini kati ya Julai na Oktoba, mwaka huu.
Kati ya fedha hizo, Sh38.6 bilioni zimepelekwa katika shule za msingi na Sh44.6 bilioni zimeenda katika shule za sekondari ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa utoaji elimu bila malipo.
Taarifa ya utolewaji wa fedha hizo imetolewa jana (Novemba 16, 2018) bungeni Jijini Dodoma wakati Waziri Mkuu Kassimu Majaliwa akitoa hoja ya kuahirisha mkutano wa 13 wa Bunge ambalo limehairishwa hadi Januari 29, 2019.
Majaliwa amesema tangu kuanza kutekelezwa kwa mpango wa elimu msingi bila malipo, uandikishaji watoto wa darasa la awali na darasa la kwanza umeimarika na kwamba kumekuwepo na mwenendo mzuri wa ufaulu kwenye mitihani ya kumaliza darasa la saba.
“Kumekuwepo na mwenendo mzuri wa ufaulu katika mitihani ya kumaliza darasa la saba, ambapo mwaka 2016 ilikuwa wastani wa asilimia 70 na mwaka 2018 ilikuwa ni wastani wa asilimia 78. Hali hiyo, imeongeza mahitaji mbalimbali, ikiwemo miundombinu katika shule zetu za msingi na sekondari,” amesema Majaliwa
Zinazohusiana: Benki ya dunia yaridhia kutoa mkopo wa zaidi ya 600 bilioni: Ikulu
Amesema Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu na kuweka mazingira mazuri katika mfumo mzima wa elimu nchini kwa kushirikiana na wadau wote.
“Kwa mfano, kupitia programu ya Lipa Kulingana na Matokeo katika Elimu (EP4R), shilingi bilioni 53.4 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya shule za msingi na sekondari. Aidha, shilingi bilioni 9.2 zimeelekezwa katika uimarishaji wa miundombinu ya elimu kupitia programu ya kuboresha elimu ya shule za msingi (EQUIP-T),” amesema Majaliwa.
Pia ameziagiza taasisi zote zinazohusika na usimamizi na uendeshaji wa mitihani ya Taifa hazina budi kuhakikisha zinasimamia kikamilifu mitihani hiyo ili kuepuka wizi na udanganyifu.
“Itakapobainika kuwepo kwa udanganyifu wa mitihani, hatua stahiki zichukuliwe kwa mujibu wa sheria dhidi ya yeyote atakayehusika,” amesisitiza.
Latest
