Sh127.3 bilioni za IFAD kukuza sekta ya kilimo Tanzania

May 20, 2019 3:03 pm · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link

Mfuko wa IFAD umekuwa ukitoa pesa na misaada mbalimbali katika sekta ya kilimo duniani ikiwa ni hatua ya kuwainua wakulima na kuziwezesha nchi zinazotegemea kilimo kufaidika na sekta hiyo. Picha|IFAD.


  • Fedha hizo zitatumika kutekeleza miradi ya kilimo kwa miaka mitatu kuanzia mwaka 2020. 
  •  IFAD inaisubiri Tanzania iainishe maeneo mahususi ya miradi ya kilimo ambako fedha hizo zitaelekezwa.
  • Rais Magufuli amesema fedha hizo zitatumika kuzalisha mbegu bora za mazao na kutatua changamoto ya masoko. 

Dar es Salaam. Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) umesema unaisubiri Tanzania kuainisha maeneo mahususi ya miradi ya kilimo ambayo yatafaidika na ufadhili wa Sh127.3 bilioni ilizotenga kuipatia kwa miaka mitatu kuanzia mwaka 2020. 

Rais wa IFAD, Gilbert Fossoun Houngbo aliyekuwa akizungumza leo (Mei 20, 2019) Ikulu Jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo na Rais John Magufuli, amesema ikiwa miradi hiyo ya kilimo itatekelezwa kama itakavyoainishwa na Serikali itasaidia kuleta tija kwa wakulima na kukuza uchumi wa nchi. 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu,  IFAD inasubiri upande wa Tanzania kuainisha maeneo mahususi ya miradi ya kilimo ambako fedha zitaelekezwa.

Ameeleza kuwa ana matumaini miradi hiyo itafanikiwa kwa kuzingatia kuwa Tanzania ni nchi yenye amani na namna Serikali ilivyo na dhamira ya maendeleo.

Mfuko wa IFAD umekuwa ukitoa pesa na misaada mbalimbali katika sekta ya kilimo duniani ikiwa ni hatua ya kuwainua wakulima na kuziwezesha nchi zinazotegemea kilimo kufaidika na sekta hiyo.

Kwa upande wake, Rais Magufuli ameishukuru IFAD kwa ushirikiano wake mzuri kwa Tanzania na amemhakikishia Houngbo kuwa ushirikiano na uhusiano huo ulioanza mwaka 1978 utadumishwa kwa maslahi ya Watanzania.


Zinazohusiana: 


Rais Magufuli amesema fedha zilizotengwa katika mpango huo wa miaka mitatu zitaelekezwa katika maeneo yenye maslahi mapana ya sekta ya kilimo ikiwemo kuwezesha matumizi ya zana bora za kilimo, kuzalisha mbegu bora za mazao, kutatua changamoto ya masoko ya mazao na kuboresha ufugaji.

Ameipongeza IFAD kwa kutoa fedha pasipo kuweka masharti ya maeneo zinakopaswa kuelekezwa.

Hata hivyo, Rais Magufuli ameiagiza Wizara ya Kilimo kuharakisha mchakato wa kuainisha maeneo yatakayopokea fedha hizo ili utekelezaji wa mpango huo uanze.

Wakati huo huo, Rais Magufuli amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Ushirikiano wa Maendeleo ya Kimataifa wa Sweden, Peter Eriksson.

Baada ya mazungumzo hayo, Eriksson amempongeza Rais Magufuli na Serikali yake kwa mafanikio makubwa katika mapambano dhidi ya rushwa na ameeleza dhamira ya Sweden kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano wake na Tanzania.

Mazungumzo hayo yamehudhuriwa na Balozi wa Sweden hapa nchini Anders Sjöberg na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Profesa Palamagamba Kabudi.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW