Serikali yajipanga kuwapandikiza Sokwemtu katika hifadhi za Ibanda na Rumanyika
- Ikolojia ya maeneo hayo inaruhusu kustawi kwa wanyamapori hao kwa kuwa yana makazi mazuri na chakula cha kutosha.
- Ni hifadhi zilizotangazwa hivi karibuni kuwa hifadhi za Taifa na Rais wa John Magufuli.
- Hatua hiyo itachochea utalii na ukuaji wa pato la Taifa.
Dar es Salaam. Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamis Kigwangalla amesema watawapandikiza Sokwemtu katika hifadhi za Taifa za Rumanyika Orugundu na Ibanda za mkoani Kagera kwa kuwa hifadhi hizo zina mazingira mazuri na chakula cha kutosha kinachoruhusu kustawi kwa wanyamapori hao.
Hatua hiyo itachangia kukuza shughuli za utalii wa Sokwemtu hapa nchini na kuongeza pato la Taifa linalotoka katika sekta ya utalii.
Taarifa ya Wizara ya Maliasili na Utalii iliyotolewa leo (Julai 13, 2019) imeeleza kuwa Dk Kigwangalla ametoa kauli hiyo mkoani Kagera wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya shughuli za uhifadhi katika hifadhi hizo zilizotangazwa hivi karibuni kuwa hifadhi za Taifa na Rais John Magufuli.
Hifadhi za Taifa za Rumanyika Orugundu inapatikana wilayani Karagwe ambapo ile ya Ibanda iko Wilaya ya Kyerwa, mkoani Kagera.
Zinazohusiana:
- Tanzania yaangazia masoko 18 duniani kukuza utalii
- Tanzania yang’ara tena tuzo za eneo bora la utalii duniani
Waziri huyo amesema mpango huo umekuja kufuatia taarifa za kitaalam kuonyesha kuwa katika miaka mingi iliyopita kulikua na Sokwemtu katika maeneo hayo ya wilaya ya Kyerwa na Karagwe.
Amebainisha kuwa ikolojia ya maeneo hayo inaruhusu kustawi kwa wanyamapori hao kwa kuwa yana makazi mazuri na chakula cha kutosha.
Wahifadhi wakiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Rumanyika Orugundu wilayani Karagwe wakati wa ziara ya Kikazi ya Waziri wa Maliasili na Utalii Dk Hamis Kigwangalla katika hifadhi hiyo. Picha| Wizara ya Maliasili na Utalii.
Latest