Serikali ya Tanzania mbioni kutunga sheria za uwekezaji
- Sheria hizo zinakwenda sambamba na mpango wa kuboresha mazingira ya biashara nchini.
- Zitasaidia kutatua changamoto za biashara na uwekezaji nchini.
- Yaitaka sekta binafsi kutoa maoni na mapendekezo kuboresha sheria hizo.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imewataka wadau wa sekta binafsi nchini kuendelea kutoa maoni na mapendekezo yao ya kitaalamu kuhusu rasimu ya Sheria ya Uwezeshaji Biashara inayolenga kuweka mazingira wezeshi yatakayochochea ukuaji wa biashara na uchumi nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya uwekezaji, Angellah Kairuki aliyekuwa akizungumza na menejimenti ya wafanyakazi wa kampuni ya sigara Tanzania (TCC), amesema Serikali imekusudia kukusanya maoni ili kuhakikisha inatunga sheria imara itayosaidia kukuza na kuimarisha sekta ya biashara nchini.
Katika taarifa iliyotolewa leo na Idara ya Habari-Maelezo, Waziri huyo amesema sekta binafsi ni wadau muhimu wanaopaswa kutoa mapendekezo, maoni na uzoefu walionao kwa kuzingatia aina ya biashara na mifumo ya kisheria iliyopo nchini.
“Serikali imeamua kuja na sheria mpya itayohusika na biashara peke yake na hili tutakusudia kuangalia ni maeneo yapi yanapaswa kuboreshwa ikiwemo masuala ya kisera, kisheria na kikanuni ili kuziweka katika eneo moja na pale kwenye changamoto tufanye marejeo na marekebisho,’’ amesema Waziri Kairuki.
Zinazohusina:
- Kiswahili ndiyo mpango mzima kusaka wateja Tanzania: Ripoti
- Sababu zilifanya Tanzania iporomoke viwango vya ufanyaji biashara duniani
Kwa mujibu wa Kairuki, rasimu ya Sheria ya Uwezeshaji Biashara imekusudia kwenda sambamba na mpango wa kuboresha mazingira ya biashara nchini (Blue Print) ambapo sekta ya biashara inatajwa kuwa kiungo muhimu katika ufanikishaji wa mpango huo.
Serikali inategemea kwa kiasi kikubwa maoni na mapendekezo ya wafanyabiashara katika kuweka mazingira wezeshi ya kuimarisha sekta ya biashara nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki akitazama moja ya chupa inayozalishwa katika Kiwanda cha Kioo Ltd wakati wa ziara yake ya kutembelea Ofisi za Kiwanda hicho jana (Desemba 16, 2019). Picha|Habari-Maelezo.
Katika hatua nyingine, Kairuki amesema Serikali itaendelea kulinda viwanda vya ndani ili kuhakikisha kunakuwa na mnyororo wa thamani kwa kuongeza kasi ya ununuzi wa malighafi na kupanua masoko ya bidhaa za ndani na nje ya nchi.
Aliongeza kuwa sambamba na kutunga Sheria ya Uwezeshaji Biashara, Serikali pia imeanza mchakato wa kutunga sheria ya uwekezaji inayolenga katika kubainisha vikwazo na changamoto mbalimbali zinazowakabili wawekezaji nchini.
‘Hapa katika Sheria hii tumeamua kuja na mpango maalum wa kujua ni wapi One-Stop center (vituo vya pamoja) iwepo, nini kinahitaji, changamoto za vibali pamoja na masuala mengione muhimu ambayo ni muhimu katika usimamizi kwa wawekezaji wetu nchini na kama mambo yatakaa vizuri katika Bunge lijalo tutaanza mchakato wake,’’ amesema.
Latest