Serikali ya Misri kutengewa eneo bandari ya Bagamoyo, Kwala
- Yaahidi kushirikiana kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo uchukuzi, nishati, afya na kilimo.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imesema itatenga eneo maalum Bandari ya Bagamoyo na Bandari ya Kwala zilizopo mkoani Pwani kwa ajili ya Serikali ya Misri kujenga eneo maalum la kuhifadhi mizigo.
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliyekuwa akizungumza leo Julai 18, 2016 Ikulu ya Dar es Salaam baada ya mazungumzo na Rais wa Misri Abdel Fattah El-Sisi, amesema uamuzi huo ni sehemu ya kuimarisha uhusiano wa nchi hizo katika sekta za uchukuzi.
“Tumekubaliana kuunganisha bandari zetu…(Misri) wataunganisha Bandari na reli kwenda Kwala ambako tutawapatia eneo la kuweka bidhaa na makontena yao,” amesema Rais Samia.
Uwekezaji wa Misri katika bandari hizo mbili unakuja wakati ambao Serikali inaendelea kuwekeza na kuboresha miundombinu ya kimkakati ya usafirishaji ili kuifungua nchi kiuchumi, kuongeza ushindani wa biashara na kuunga mkono azma ya Tanzania kufikia uchumi wa Dola za Marekani trilioni moja ifikapo mwaka 2050.
Tangu kuanzishwa kwake, bandari hizo zimekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha huduma za usafirishaji nchini, iikiwemo kusaidia kupunguza msongamano katika Bandari ya Dar es Salaam, kuongeza uwezo wa kuhifadhi mizigo na kuboresha mnyororo wa usafirishaji.
Kwa upande wake, Rais wa Misri Abdel Fattah El-Sisi, amesema nchi yake iko tayari kushirikiana na Tanzania katika kuendeleza miundombinu ya kimkakati, ikiwemo maeneo ya bandari, ili kukuza biashara na kuunganisha masoko ya Afrika.
Licha ya uwepo wa uwekezaji baina ya nchi hizo unaofikia zaidi ya Sh1 bilioni na kutoa ajira kwa zaidi ya Watanzania 4,000 Rais Samia amesema Tanzania na Misri zina nafasi kubwa ya kupanua uwekezaji huo.

Air Tanzania kuruka Misri
Wakati Serikali hizo zikijipanga kuimarisha sekta ya uchukuzi majini na ardhini, Rais Samia Suluhu Hassan amegusia pia maandalizi ya Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kuanza safari rasmi nchini Misri.
Hatua inayotarajiwa kufungua njia mpya za usafiri wa abiria na mizigo pamoja na kuchochea zaidi uhusiano wa kiuchumi na kindugu kati ya mataifa hayo mawili.
“Tumejadiliana na kukubaliana kwamba EgyptAir inakuja mara tatu kwa wiki ndani ya Tanzania hivyo ‘Air Tanzania (ATCL)’ nayo mjiaandae kutoa huduma kama hiyo kuelekea miji kule nchini Misri
Aidha, viongozi hao pia wameshuhudia utiaji saini wa rasimu ya makubaliano kuhusu ushirikiano katika sekta mbalimbali za uchukuzi pamoja na makubaliano ya ushirikiano katika sekta ya uchukuzi.
Pia,Tanzania zimekubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta za kilimo cha mazao na mifugo, usafi nishati, ujenzi, viwanda na utalii.