Serikali: Wapangaji wanaolipa kodi ya zuio kwa ajili ya pango wanatakiwa kurejeshewa fedha zao
- Waziri wa fedha asema kodi hiyo anafaa kuilipa mwenye jengo.
- Mpangaji hutumika kama wakala wa kukusanya kodi hiyo ya Serikali.
Dar es Salaam. Iwapo wewe ni miongoni mwa watu ambao hulipa kodi ya zuio kwa ajili ya kupanga nyumba au jengo la biashara, Serikali imesema mwenye nyumba anatakiwa kukurejeshea kiasi cha fedha ulizolipa na si vinginevyo.
Kwa mujibu sheria za kodi nchini Tanzania mpangaji wa nyumba ya biashara husajiliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kuwa wakala wa ukusanyaji wa Kodi ya Zuio (Withholding Tax) hivyo kuwa sehemu ya mlipaji wa kodi ya pango.
Sheria ya Kodi ya Mapato inamtaka mmiliki wa nyumba ya biashara mwenye mapato yanayozidi Sh500,000 kulipa kodi ya zuio kutokana na mapato yanayotokana na upangishaji wa pango (rental tax) kwa kiwango cha asilimia 10 ya mapato ya kodi ya pango husika
Hata hivyo baadhi ya wapangaji ambao hulipa kodi hiyo huwa hawarudishiwi fedha hizo ambazo walitakiwa kukatwa wapangishaji ikiwemo hata kufidiana kwenye kodi.
Waziri wa Fedha na Mipango Dk Philip Mpango ameliambia Bunge leo kuwa kodi hiyo ya zuio siyo ya mpangaji, na kwa kuwa Sheria ya Kodi ya Mapato inamtambua mpangaji kama wakala, kiasi cha kodi ya pango ambacho kimelipwa na mpangaji huhesabiwa kama sehemu ya fedha ambazo anapaswa kurejeshewa na mwenye nyumba.
“Kwa mujibu wa Sheria ya Kodi ya Mapato, mpangaji ambaye sio mfanyabiashara na hajasajiliwa na TRA kama mlipakodi hapaswi kukusanya kodi hii”, amesema Dk Mpango wakati akijibu swali la Mbunge wa Babati Mjini, Pauline Gekul jijini Dodoma.
Soma zaidi:
- Serikali kuwabana wanaopangisha nyumba kwa watalii bila leseni
Gekul alitaka kujua lini Serikali itabadili utaratibu wa kumtoza mpangaji wa nyumba ya biashara kodi ya zuio ya asilimia 10 badala ya mpangishaji.
Dk Mpango amesema kuwa utaratibu wa ukusanyaji Kodi ya Zuio kupitia wakala ambaye ni mpangaji umewekwa ili kurahisisha ukusanyaji wa kodi hiyo, hususan pale mpangishaji anapokuwa hajasajiliwa na TRA kama mlipa kodi.