Sababu za TRA kuvunja rekodi ya ukusanyaji Sh1.7 trilioni Septemba
- Imekusanya Sh1.7 trilioni kwa mwezi mmoja, kiasi ambacho hakijawahi kukusanywa na mamlaka hiyo tangu ianzishwe.
- Kuzibwa kwa mianya ya ukwepaji kodi, msisitizo katika utumiaji wa mashine za kutolea risiti za (EFD) vimesaidia ongezeko la mapato.
- Hata hivyo, makusanyo hayo ni chini ya lengo la kukusanya Sh1.8.
Dar es Salaam. Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA), Dk Edwin Mhede ameeleza sababu mbalimbali zilizochangia kuvunja rekodi ya ukusanyaji wa mapato ya Sh1.7 trilioni mwezi Septemba mwaka huu, ikiwa ni pamoja na kuziba mianya ya ukwepaji kodi kwa kusimamia kikamilifu sheria za kodi.
Dk Mhede aliyekuwa akizungumza jana (Oktoba 1, 2019) jijini Mbeya amesema makusanyo hayo ya mwezi uliopita yamevunja rekodi kwa sababu mamlaka hiyo haijawahi kukusanya kiasi kama hicho katika miaka iliyopita.
Kiasi kilichokusanywa kwa mwezi Septemba cha Sh1.7 trilioni ni sawa na ufanisi wa asilimia 97.20 ya lengo la awali la ukusanyaji wa Sh1.8 trilioni kwa mwezi husika.
Ufanisi na ongezeko la makusanyo hayo ni mwendelezo wa makusanyo yaliyopatikana tangu kuanza kwa mwaka mpya wa fedha wa 2019/20 ulioanza Julai 1 mwaka huu.
Kwa mujibu wa TRA, wezi Julai ilikusanywa Sh1.25 trilioni ikiwa ni sawa na ufanisi wa asilimia 91.9 ya lengo la ukusanyaji wa mapato na mwezi uliofuata wa Agosti walikusanya Sh1.33 trilioni kabla ya kupaa kwa kasi hadi Sh1.7 trilioni mwezi uliopita.
Akizungumzia rekodi hiyo ya Septemba, Dk Mhede amesema imechangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo wananchi kuelewa umuhimu wa ulipaji kodi lakini vilevile mikakati iliyowekwa na TRA kuhakikisha lengo kuu linafikiwa.
#TAARIFA BOFYA HAPA KUTAZAMA TAARIFA YA MAKUSANYO TRA https://t.co/pZyZEsVQHs
— TRA Tanzania (@TRATanzania) October 1, 2019
Badhi ya mikakati hiyo ni pamoja na kuziba mianya ya ukwepaji kodi kwa kusimamia kikamilifu sheria za kodi, kuweka msisitizo katika utumiaji wa mashine za kutolea risiti za (EFD), kutoa elimu kwa mlipakodi, ujengaji wa mifumo rafiki ya ukusanyaji kodi na uboreshaji wa huduma za mlipakodi.
Hata wakati TRA ikivunja rekodi ya makusanyo kwa mwezi wa Septemba, mamlaka hiyo haijaweza kufikia lengo la makusanyo kwa miezi yote mitatu iliyopita ya robo ya kwanza ya mwaka wa fedha wa 2019/2020.
Mathalani, Septemba walipanga kukusanya Sh1.8 trilioni lakini wamefanikiwa kukusanya Sh1.7 trilioni ikiwa ni upungufu wa takribani Sh1 bilioni ya lengo husika.
“Pamoja na mafanikio haya, tunajua bado hatujafikia lengo letu. Aidha, TRA tunatambua kuwa mafanikio haya yanakuja na changamoto. Ni lazima wote, yaani walipa kodi na watendaji wa TRA tukabilian na changamoto hiyo na tushinde,” amesema Dk Mhede.
Katika hatua nyingine, bosi huyo wa TRA amewaasa wale wote wanaojishughulisha na vitendo viovu vya kughushi risiti za kielektroniki (EFD) kuacha mara moja kwa sababu wanafanya operesheni maalum kuwabaini.