Sababu Apple kuwazuia wafanyakazi wake kutumia ChatGPT

June 20, 2023 1:35 pm · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Yahofia taarifa zake muhimu kuvuja na kutumika isivyo halali.


Dar es Salaam. Kampuni ya Apple ya Marekani imewazuia wafanyakazi wake kutumia zana za akili bandia (AI) ya ChatGPT ya OpenAI kwa kuhofia taarifa za siri zake zinazoingizwa katika mifumo hiyo zinaweza kuvuja au kuchukuliwa. 

Kwa mujibu wa taarifa kutoka jarida la The Wall Street Journal, wafanyakazi wa Apple wameonywa pia kutumia programu saidizi ya GitHub.

Mwandishi wa habari wa shirika la habari la Bloomberg, Mark Gurman katika ukurasa wake wa Twitter amesema ChatGPT imekuwa ni miongoni mwa programu zilizozuiliwa na kampuni hiyo kwa miezi sasa.

Kampuni hiyo inayotengeneza simu za iPhone inaweza kuwa na sababu za msingi kwa uamuzi iliouchukuwa ikizingatiwa kuwa OpenAi inatunza taarifa na mazungumzo yote kati ya mtumiaji na ChatGPT. 

Mazungumzo hayo yanakusanywa ili kuifundisha mifumo ya OpenAI inayomilikiwa na kampuni ya Microsoft na yanaweza kuingiliwa na kutumika visivyo. 

Aprili mwaka huu, OpenAI ilizindua kipengele ambacho kinawaruhusu watumiaji wake kuzuia historia ya mazungumzo yao  (siku chache baada ya mataifa mengi ya Ulaya kuanza kuchunguza zana hiyo kama inavunja faragha za masingi).

Licha ya kipengele hicho, OpenAI inatoa fursa ya mazungumzo kukaa kwa siku 30 kabla haijayafuta kabisa ili kuimarisha faragha na usiri. 

Ikizingatiwa kuwa ChatGPT inapewa kazi mbalimbali ikiwemo kuchakata mawazo, Apple inahofia kuwa wafanyakazi wake wanaweza kuingiza taarifa za siri za miradi yake katika mfumo huo ambao unatajwa kuwa ni mapinduzi makubwa ya mawasiliano.

Siyo Apple pekee imeweka zuio hilo. Kampuni nyingine kama JP Morgan, Verizon, na Amazon zimechukua hatua kama hiyo. 

Licha ya zuio hilo, imeruhusu OpenAi kuzindua programu tumishi (iOS app) ya ChatGPT inayotumia mfumo endeshi wa Apple (iOS).

 OpenAI imesema itawezesha app hiyo kutumika katika nchi nyingine zaidi ya Marekani sambamba na app ya Android. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW