Tamaduni zinavyodumaza vipaji wa wasichana mkoani Mwanza

Mariam John 0708Hrs   Januari 18, 2024 Ripoti Maalum
  • Wasema michezo inasababisha wasichana kuwa wahuni.
  • Baadhi ya wazazi wasema ni utamaduni huo umepitwa na wakati.
  • WHO yabainisha hatari za kiafya ikiwa mtoto hatashiriki michezo.

Mwanza. Wakati juhudi mbalimbali zikiendelea kumkomboa msichana katika mila na tamaduni zisizofaa, baadhi ya jamii mkoani Mwanza bado zinawazuia watoto wa kike kushiriki michezo jambo linaloweza kuathiri vipaji na afya zao.

Katikati ya jamii hiyo, Asha Kusasa mwanafunzi wa darasa la saba katika Shule ya msingi Mwanhengele wilayani humo anazuiwa kutimiza ndoto zake za kuwa mchezaji wa mpira wa miguu kutokana na imani ya kwamba wanaocheza mchezo huo ni wahuni.

Mwanafunzi huyo anaeleza kuwa mapenzi yake na mchezo huo wa mpira wa miguu yalianza pale wakati akitaza mchezo huo kupitia runinga na baadae kutamani kushiriki katika mashindano ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Msingi Tanzania (Umitashumta).

"Toka mwanzo ninapenda kucheza mpira na hata nikiwa naangalia runinga napendelea zaidi kutazama mpira wa miguu,hali hiyo ilinipa haja ya kujiingiza kwenye michezo wa aina hii," amesema Asha.

Ndoto ya Asha inapata matumaini pale ambapo Mwalimu wa Mkuu wa shule hiyo, Ernest Malima alipofanikisha kumuombea ruhusa Asha kushiriki michezo hiyo  baada ya kuona kipaji chake.

“Mwalimu wa michezo aliona kipaji cha mchezo kwa Asha, na baada ya kupewa mafunzo alikuwa ni mtoto mwenye kipaji cha kucheza mpira wa miguu lakini mwanzoni wazazi hawakutaka ashiriki kutokana na imani yake kutoruhusu maungo yake kuwa wazi," amesema Malima.


Soma zaidi:Si kweli: Mtu ajirusha ghorofa ya nne hoteli ya bondeni Magomeni Tanzania


Hata hivyo, Mwalimu huyo anakutana na ugumu wakati wa kumuombea Asha ruhusua kutokana na wazazi hao kuamini kuwa binti yao akicheza michezo ataajiingiza kwenye uhuni na kushindwa kuzingatia masomo.

"Kwa kiasi fulani wazazi walikubali na kumruhusu Asha kujiunga na michezo ya Umitashumta ambapo alifanikiwa hadi kufika ngazi ya taifa na kurudi na zawadi," amesema Malima.

Wakati Asha akipambania ndoto yake huku akiimarisha afya  Shirika la Afya Duniani (WHO) linaainisha mdhara ya watoto chini ya umri wa miaka 18 kuwa ni magonjwa ya moyo, uzitouliopitiliza pamoja na msongo wa mawazo.

Pia, WHO wamebainisha kuwa ushiriki wa watoto wa kiume katika michezo unatakiwa kwenda sambamba na ushiriki wa watoto wa kike ili waweze kupata faida sawa za kiafya.

“Mwenendo wa wavulana kushiriki michezo zaidi ya wasichana unashtua …jitihada zaidi zinahitajika kukidhi mahitaji na maslahi ya wasichana  ili kuwavutia kuendeleza ushiriki wao katika shughuli za kimwili ikiwemo michezo,” imesema ripoti ya Shirika hilo.

Makamu wa Rais  Dkt. Philip Mpango akiwakabidhi mipira baadhi ya manahodha wa timu za michezo mbalimbali mara baada ya kufungua rasmi Mashindano ya UMITASHUMTA  na UMISSETA yaliyofanyika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi Mkoani Tabora tarehe 06 Juni 2023.PichaMichuzi blog.

Ni mila iliyopitwa na wakati

Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wazazi katika kata ya Mwanhengele wamesema wapo ambao wanazuia watoto wao wasishiriki michezo wakimini kuwa ni uhuni lakini tamaduni hiyoimepitwa na wakati.

"Nikiri tu kuwa mila na desturi za aina hiyo zimeshapitwa na wakati, tunashudia kwa sasa wachezaji wengi wa kike wakishiriki michezo mbalimbali ikiwemo ya mpira wa miguu na wanalipwa kupitia michezo hiyo," amesema  Makoye Lunyilija mkazi wa Mwanhengele.

Lunyilija anasema wazazi wengi wanataka watoto wao wa kike wasome na wengine wawaozeshe wapate mahali  lakini masuala ya mpira huwa hayapewi kipaumbele.

Mzazi mwingine, Ester Samweli amesema sio wazazi wote wanazuia watoto wasishiriki michezo wengine wanatamani  kuona watoto wao wakionyesha vipaji vyao.

"Tunatamani kuona watoto wapewe uhuru wa  kushiriki kile ambacho wanatamani kukifanya hii itawajengea uwezo na kujiamini zaidi kwenye masomo yao na hata wawapo kwenye jamii," amesema Ester.


Soma zaidi:Watoto wadogo katikati ya safari ya kuisaka elimu madarasa ya awali Tanzania


Amefafanua kuwa  kinachowapa hofu wazazi ni  hapo zamani hakukuwa na watoa huduma za afya kwa wachezaji wa kike na inapotokea mtoto wa kike amepata shida uwanjani atahudumiwa na nani.

Hali hiyo imebadilika siku za hivi karibuni kutokana na uwepo wa walimu na wahudumu wengi wa afya wanawake wanaoweza kuwasaidia wachezaji hao wakiumia wakati wa michezo au mazoezi.

Kwa mujibu wa Makamu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, Alex Nkengenye amesema tofauti na miaka ya nyuma kwa sasa wanasajii walimu na makocha wengi wa kike.

Amesema asilimia 30 ya wadahiliwa katika Chuo hicho ni wanawake ambao huchukua kozi mbalimbali ikiwemo, ya ualimu wa michezo, ukocha, uamuzi na urefa ambao wanafundisha michezo katika ngazi zote husasani watoto wadogo.

Suala la mabadiliko ya mfumo wa ukuaji pia kwa mtoto wa kike pia linachangia wazazi wasiwaruhusu wakiamini kuwa watabadilika na kuwa na mfanano wa kiume.

Viongozi wa dini wasawazisha

Wakati sintofahamu hiyo ikiendelea, Sheikh Hamza Makuza  ambaye ni miongoni wa viongozi wa dini ya Kiislam mkoani Mwanza, amesema suala la watoto wa kike kushiriki michezo ya mpira wa miguu linaruhusiwa ila hawapaswi kuacha maungo yao wazi.

Akitolea mfano wa baadhi ya wachezaji wa timu za mpira wa miguu kwa wanawake wa Simba na Yanga amesema wapoi ambao wanapokuwa uwanjani wanavaa kilemba kichwani (ushungi) na jezi zao zinakuwa na mikono mirefu.

" Kiimani inaruhusiwa kabsa mtoto wa kike kushiriki michezo ya aina yoyote ingawa tu anapoingia uwanjani atalazimika kujifunga kilemba, jezi zake itakuwa kwenye mfumo wa ‘truck suti’ yaani suruali na jezi ya mikono mirefu," amesema Makuza.

Related Post