Hifadhi ya Katavi; mahali unapoweza kushuhudia mapigano ya viboko na mamba
- Asili yake imetokana na mwindaji maarufu wa kienyeji aliyeishi katika maeneo hayo ya hifadhi akijulikana kama “KATABI”
- Kivutio kikubwa cha hifadhi hiyo ni mapigano ya makundi ya viboko na mamba kwenye Ziwa Katavi.
- Inafikika mwaka mzima kwa kutumia magari ya kukodi, treni na ndege.
Dar es Salaam. Unapozitaja au kuzungumzia hifadhi za taifa Tanzania, basi hutaacha kuitaja Ruaha na Serengeti kutokana na umaarufu wake wa kutembelewa na watalii wengi kutoka nje ya nchi.
Umewahi kuisikia Hifadhi ya Taifa ya Katavi? Hii ni hifadhi ya tatu kwa ukubwa nchini baada ya Ruaha na Serengeti ambapo imesheheni vivutio vingi ambavyo huwezi kuvikuta katika maeneo mengine duniani.
Ina ukubwa wa kilomita za mraba 4,471 na inapatikana katika wilaya ya Mpanda mkoa wa Katavi ambapo ni miongoni mwa hifadhi tano zinazopatikana Kusini Magharibi mwa Tanzania karibu na Ziwa Tanganyika .
Kwa mujibu wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Katavi ilitangazwa kuwa Hifadhi ya Taifa mwaka 1974 ikiwa na ukubwa wa kilometa za mraba 2,253 na ilipofika 1996 iliongezwa eneo na kufikia kilometa za mraba 4,471.
Jina la hifadhi hiyo limetokana na jina la asili la mwindaji maarufu wa kienyeji aliyeishi katika maeneo hayo ya hifadhi akijulikana kama “KATABI”. Pia watu wanaamini Katabi ni mzimu maarufu wa kabila la Wabende ambapo mpaka leo watu wanafika katika eneo hilo na kuelekea kwenye mti ulipo Ziwa Katavi wakiamini mzimu huo ulikuwa unaishi hapo kabla ya hifadhi.
Inaaminika mzimu wa Katabi una uwezo wa kufanya miujiza mbalimbali kama kunyesha kwa mvua, kutatua shida na changemoto mbalimbali hata kuzuia magonjwa ya mlipuko kama ndui.
Kiboko akiwa na mambo, ni kivutio kikubwa katika Hifadhi ya Taifa ya Katavi. Picha| Jamii moja
Kufika kwako katika Hifadhi ya Taifa ya Katavi kutakupa fursa ya kujionea wanyama pori wengi yakiwemo makundi makubwa ya tembo , nyati, simba , pundamilia , mbwa mwitu , kongoni, swala pala na nyemela.
Huku eneo la mto Stalike na Iku ikiwa ni kivutio kikubwa cha utalii kutokana na mapigano ya makundi ya viboko na mamba. Pia utakutana na idadi kubwa ya vipepeo na ndege wa aina mbalimbali.
Achilia mbali uwepo wa wanyama kuna mandhari pana ya uwanda tambarare wa nyasi katika mkondo wa bonde la ufa la Rukwa. Uoto huo wa asili unakupatia aina 226 za miti na mito na vijito zikiingia na kutoka katika eneo la hifadhi.
Hifadhi hii inafikika mwaka mzima kwa kupitia Mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza , Kigoma Arusha hadi Mpanda kupitia Tabora kwa kutumia usafiri wa ndege za kukodi “Chartered Planes” au kwa njia ya barabara kupitia mkoa wa Mbeya na Rukwa.
Kwa wanaopendelea usafiri wa treni wanaweza kufika kutoka popote walipo ikiwa watapanda treni katika mji wa Tabora .
Vitu ambavyo mtalii anawezafanya kwenye hifadhi.
Mtalii akiwa hifadhi hiyo anaweza kutazama wanyama kwa kutumia gari hasa nyakati za asubuhi ambapo wanyama wanakuwa wamepumzika. Pia matembezi mafupi yanayojulikana kama “Sitalike walking Trail” kuanzia kilomita moja hadi hadi tisa.
Kwa wanaopenda kutembea basi yapo matembezi marefu (Chorangwa Hiking Trail) ya kilomita 10 na kuendelea ambapo mtalii ana uwezo kutembea kwa saa 10.
Pia ndani ya hifadhi ya Katavi, mtalii anaweza kufanya utalii wakati wa usiku kumuwezesha kuona wanyama ambao mchana hawaonekani kirahisi akiwa kwenye gari la wazi na lenye taa maalumu.
Kuweka kambi ndani ya hifadhi hiyo nayo ni huduma nyingine ambayo hutaikosa ukiwa kwenye hifadhi ya Katavi.
Latest