Rais Magufuli ziarani nchini Malawi

April 24, 2019 11:20 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link

Rais John Magufuli akisalimiana na Rais wa Malawi, Arthur Peter Mutharika. Picha| Mtandao.


  • Akiwa Malawi atakutana na kufanya mazungumzo na Rais Peter Mutharika na kufungua msimu mpya wa soko la tumbaku.
  • Rais Magufuli atarejea nchini na ataanza ziara ya kikazi ya siku nane katika mkoa wa Mbeya.

Dar es Salaam. Rais John Magufuli ameondoka leo nchini kwenda Malawi kwa ziara ya siku mbili ambayo itahusisha shughuli mbalimbali ikiwemo kukutana na kufanya mazungumzo na mwenyeji wake Rais Arthur Peter Mutharika. 

Ziara hiyo huenda ikafungua fursa nyingi na kuimarisha mahusiano ya kibiashara kati ya nchi hizo mbili ambazo zimetenganishwa na Ziwa Nyasa katika mikoa ya Mbeya na Ruvuma. 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu leo (Aprili 24, 2019( ,Gerson Msigwa imesema Rais Magufuli ameongozana na mkewe Mama Janeth Magufuli na atafanya ziara ya siku mbili kwa mwaliko wa Rais wa Jamuhuri ya Malawi Profesa Arthur Peter Mutharika .

Akiwa nchini humo Rais Magufuli anatarajia kuweka shada la maua katika mnara wa kumbukumbu ya aliyekuwa Rais wa Malawi Hayati Bingu Mutharika pia atafanya mazungumzo na mwenyeji wake Rais Mutharika na baadaye kuhudhuria dhifa ya kitaifa iliyoandaliwa kwa heshima yake.

Katika siku ya mwisho ya ziara yake, Rais Magufuli atafungua msimu wa soko la tumbaku pamoja na mwenyeji wake na kuzungumza na wadau wa zao hilo. 


Soma zaidi: Magufuli kuzuru Mwanza, Simiyu, Mara kwa siku saba


Tumbaku imekuwa zao muhimu la biashara kwa nchi hizo mbili ambapo kwa Tanzania, tumbaku ni zao la pili linaloingiza fedha nyingi za kigeni baada ya korosho.

Kwa mujibu wa Kitabu cha Hali ya Uchumi wa Taifa (2017) kilichotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) katika kipindi hicho cha mwaka mmoja, tumbaku iliingiza kiasi cha Sh430 bilioni. 

Malawi nayo nayo ni miongoni mwa nchi zinazozalisha tumbaku kwa wingi duniani. Uchumi wa nchi hiyo iliyoko kusini mwa bara la Afrika unategemea kilimo cha zao hilo kwa asilimia 75.

Kwa mujibu wa Tume ya udhibiti wa Tumbaku (TCC), Wakulima wa tumbaku nchini Malawi hawaruhusiwi kuuza wenyewe tumbaku yao kwa namna yoyote, bali wanapaswa kujiunga kwenye vikundi vidogo vidogo na kuipeleka katika mnada maalum wa tumbaku unaosimamiwa na shirika la Umma la Auction Holdings.

Katika minada hiyo ya pamoja wanakutana na wanunuzi ambao ni makampuni makubwa ya kimataifa yakiwemo ya  Alliance One, Japan Tobacco na Malawi Leaf.

Baada ya ziara hiyo Rais Magufuli atarejea nchini ambako ataanza ziara ya kikazi ya siku nane katika mkoa wa Mbeya ikiwemo kuhudhuria sikukuu ya wafanyakazi ya Mei Mosi. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW