NHIF yafanya maboresho kitita cha huduma za afya
- Utekelezaji wake utaanza Machi 1, 2024.
- Yamegusa huduma za usajili na kupata ushauri wa daktari.
Dar es Salaam. Huenda watumiaji wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) wakapata ahueni katika huduma za afya hivi karibuni mara baada ya mfuko huo kutangaza kufanya maboresho katika kitita cha mafao ya huduma ya afya kwa wanufaika wake.
Kitita cha mafao ni orodha ya huduma za matibabu ambazo zinatolewa kwa wanufaika wa NHIF na bei zake ambazo hutumika wakati wa malipo kwa madai ya watoa huduma za matibabu.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mkurugenzi wa NHIF Bernard Konga iliyotolewa leo Februari 28, 2024 maboresho hayo yatahusisha vipengele vitatu ambavyo utekelezaji wake unatarajia kuanza Machi Mosi mwaka 2024.
Taarifa ya Konga inafafanua kuwa kipengele cha kwanza kilichofanyiwa maboresho ni huduma za usajili na kupata ushauri wa daktari ambapo yatasaidia kuweka usawa wa ada ya kumwona daktari kwa ngazi zote kwa madaktari wa kada zinazoendana.
“Hii itawezesha wanachama kupata huduma za kibingwa katika ngazi mbalimbali za vituo kwa kuzingatia uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika sekta ya Afya,” imeeleza taarifa ya Konga.
Kipengele cha pili kilichofanyiwa maboresho ni huduma za dawa ambapo dawa 736 zimefanyiwa mapitio huku nyingine mpya 247 zilizopo katika Mwongozo wa Orodha ya Dawa Muhimu za Taifa (NEMLIT) zimeongezwa
Maboresho hayo yanatarajiwa kuongeza wigo wa upatikanaji wa dawa kwa wanachama pamoja na upatikanaji wa huduma za dawa katika vituo vya ngazi ya msingi mfano dawa za shinikizo la damu na kisukari.
Aidha, maboresho mengine yamefanyika katika huduma za upasuaji na Vipimo ambapo gharama 311 za vipimo na huduma za upasuaji zimefanyiwa mapitio kwa kuzingatia bei za soko katika ununuzi wa vifaa na vitendanishi.
Kupitia kipengele hiki Konga amesema upatikanaji wa huduma za matibabu ya saratani, upasuaji wa mifupa, upasuaji wa moyo katika hospitali si za Taifa tu bali hata hospitali za kanda utaongezeka hivyo kusogeza huduma karibu zaidi na maeneo ya wananchi.
Soma zaidi:Ifahamu mikoa 10 inayoongoza kwa uzazi wa mpango Tanzania
Mabadiliko hayo ya kitita cha NHIF yanakuwa ya pili kufanyika kwa mwaka huu baada ya yale ya mwezi Januari kusitishwa na Serikali kutokana na wadau wa sekta ya afya pamoja na wamiliki wa vituo binafsi vya afya kutishia kusitisha huduma ya mfuko huo kwenye hospitali zao endapo utekelezaji wake ungeanza.
Baada ya kusitishwa huko Serikali kupitia Wizara ya Afya ilitangaza kuunda tume huru iliyofanya mapitio ya maboresho yaliyofanyika.
Kwa mabadiliko haya huenda NHIF ikapunguza malalamiko lukuki kutoka kwa watumiaji wa mfuko huo yaliyotishia utekelezaji wa sheria ya bima ya afya kwa wote ya mwaka 2023 iliyoanisha sharti la lazima la kujiunga bima ikiwemo ya mfuko huo.
Licha ya maboresho hayo Vyama vya Watoa Huduma za Afya vimesema vituo vyao vitashindwa kutoa huduma za afya ikiwa utekelezaji wa maboresho hayo utafanyika.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa vyama hivyo leo Februari 28, 2024 uamuzi huo unatokana na kukosekana kwa muafaka katika mazungumzo kati yao na kamati iliyoundwa na Wizara ya Afya.
Kutokana na maamuzi hayo, vyama hivyo vimewashauri wanachama wa NHIF kuwasiliana mfuko huo ili kujua namna watakavyoweza kupata huduma hizo.