NEMC yatoa siku 90 kwa watoa huduma za afya kuboresha miundombinu ya taka hatarishi

May 16, 2024 10:35 am · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Yasema itafanya ukaguzi katika vituo vyote nchini kubaini utekelezaji wa agizo hilo.
  • Watakaokaidi kuchukuliwa hatua ikiwemo kufungiwa vituo vyao.

Dar es Salaam. Baraza la Taifa la Kuhifadhi wa Mazingira (NEMC) limetoa siku 90 kwa watoa huduma za afya kuboresha miundombinu ya kuhifadhi taka hatarishi ili kulinda wananchi na madhara yatokanayo na kuzagaa kwa taka hizo.

Kwa mujibu wa NEMC Taka hatarishi ni zile zinazopatikana baada au wakati utoaji wa huduma za afya ikiwemo nyembe, sindan, mipira ya maji na damu, madawa yaliyotumika, baadhi ya viungo, migando ya damu na nyingine zinazofanana na hizo.

Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria NEMC, Hamad Kissiwa aliyekuwa akizungumza na waandishi wa habari leo Mei 16, 2024 jijini Dar es Salaam amesema endapo watoa huduma hao hawatazingatia kanuni za utunzaji mazingira wanaweza kusababisha madhara kwa wananchi.

“Tumekuta pia taka hizo zinatupwa porini na baadhi zinachomwa kwa moto wa wazi matokeo yake zinaleta hatari kwenye maisha ya binadamu na wanyama, madhara makubwa yanayoweza kutokana na hii kulipa hasara taifa letu,” amesema Kissiwa.

Wakati NEMC ikitoa angalizo hilo, katika jamii kumeshuhudiwa kukithiri kwa utupaji hovyo wa taka hizo hatarishi katika maeneo ya umma ikiwemo fukwe jambo linaloweza kusababisha mlipuko wa magonjwa na aina nyingine za magonjwa zinazohusisha muingiliano wa bakteria au vijidudu.


Soma zaidi:Ripoti: Afya ya akili chanzo cha watu kujiua, kuua Tanzania


Watakaokaidi kukiona

Kissiwa amesema baada ya kipindi hicho walichokitoa kwa ajili ya maboresho kuisha NEMC litafanya ziara katika vituo vyote vya afya nchini na watakaokaidi watachukuliwa hatua.

“Wale wote watakao kiuka adhabu itatolewa ikiwemo hata kusimamishwa huduma zake ili waweze kufanya marekebisho kuokoa mazingira yetu afya zetu pamoja na kulinda rasilimali za nchi yetu,” amesema Kissiwa. 

Aidha, NEMC imewataka wato huduma za afya kuacha kuwatumia watoa taka wasio thibitishwa badala yake kutumia wakandarasi walioidhinishwa na Wizara ya Afya kwa kuwa wana maeneo mahususi kwa ajili ya shughuli hiyo.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW