Mauaji ya mwanaharakati wa ujangili: 11 wahukumiwa kunyongwa hadi kufa
- Walimuua Wayne Lotter, raia wa Afrika Kusuni jijini Dar es Salaam kwa kumpiga risasi mwaka 2017
- Wawili kati yao ni raia wa Burundi.
- Lotter alikuwa akishirikian ana Serikali kupambana na ujangili nchini.
Dar es Salaam. Mahakama Kuu nchini Tanzania Ijumaa iliwahukumu kifo watu 11 adhabu ya kunyongwa hadi kufa kwa mauaji ya mwanaharakati wa ujangili, Wayne Lotter zaidi ya miaka mitano iliyopita.
Mwanaharakati wa kupinga ujangili huyo, raia wa Afrika Kusini, aliuawa kwa kupigwa risasi Agosti 2017 akiwa kwenye teksi jijini Dar es Salaam.
Waliohukumiwa kunyongwa ni pamoja na Watanzania tisa na raia wawili wa nchi jirani ya Burundi.
Hukumu iliyosomwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam Desemba 2, 2022 na Jaji Laila Mgonya, imewataja waliotiwa hatiani na kuhukumiwa adhabu hiyo ni Rahma Almas, mkazi wa Mbagala B, Nduimana Ogiste, maarufu kama mchungaji na raia wa Burundi, Godfrey Salamba mkazi wa Kinondoni Msisiri A na Chambie Juma Ally, mkazi wa Kia/Boma.
Wengine ni Allan Elikana Mafue, Ismail Issah Mohammed, Leornad Phillipo Makoi, Ayoub Selemani Kiholi; Abuu Omary Mkingie, Habonimanda Augustine Nyandwi (raia wa Burundi) na Michael Dauv Kwavava.
Tanzania haijatekeleza hukumu ya kifo kwa miongo kadhaa, huenda watu hao waliotiwa hatiani watatumikia adhabu ya kukaa gerezani maisha yao yote.
Lotter alikuwa mkurugenzi na mwanzilishi mwenza wa PALMS Foundation, asasi isiyokuwa ya kiserikali ambayo ilikuwa inasaidia kutoa mafunzo kwa askari wa wanyama pori kote nchini Tanzania na kuandaa “njia ya kiintelijensia” ya kupambana na ujangili ambayo ilifanikiwa kukabiliana na usafirishaji wa wanyamapori.
Lotter wakati anauwawa alikuwa na umri wa miaka 51 alianza kufanya kazi nchini Tanzania katika shughuli za uhifadhi tangu mwaka 2008.
Latest